Faida za mashamba ya ‘ghorofa’ kwa kilimo cha mijini
MAENEO ya mijini yanakumbana na changamoto nyingi kama vile uchafuzi wa mazingira na uhaba wa mashamba kutokana na idadi kubwa ya wakazi.
Hii ikiashiria kuwa bado wenyeji wengi wa miji wanategemea chakula kutoka mashambani maeneo ambayo kwa kawaida hukuza aina mbalimbali vyakula.
Akilimali ilipozuru eneo la Denyenye, Kaunti ya Kwale ilikutana na kijana Juma Kulonda mkulima na pia mkurugenzi wa Shirika la Greehouse Bomba Farms.
Kazi yake kubwa ni kuwaleta vijana pamoja kwa ajili ya kufanikisha shughuli za uzalishaji wa chakula hususan mijini kwa kutumia mbinu za kisasa.
Anawahimiza wakazi wa miji mikuu kama vile Nairobi, Mombasa, Kisumu na Nakuru kujihusisha na kilimo cha mjini kwa kutumia mashamba ya ‘ghorofa’ almaarufu kama ‘multi storey gardens’.
Aina hii ya mashamba ni rahisi kutengeneza pia yanaweza kustawisha aina mbalimbali ya matunda na mboga katika kipande kidogo cha ardhi.
Anasema kufikia sasa idadi ya vijana ulimwenguni wenye umri wa miaka 15-24 ni zaidi ya bilioni moja.
Asilimia hii kubwa inapigania fursa chache za ajira ambazo zinapatikana.
“Wengi wao wakiwa hawana sehemu ya kuendeshea kilimo, baadhi waliobahatika wanategemea kilimo kama njia ya kutosheleza mahitaji yao ya kila siku,” asema.
Ingawa baadhi hawajafikiwa na ujuzi wa kuendesha kilimo kwa kutumia mbinu za kisasa, anaamini kuwa washikadau katika sekta za kilimo na Wizara ya Kilimo wataona haja na kuweka mikakati ili kuwafikia vijana zaidi vijijini.
Anasema wanaweza kutumika kama mabalozi wa kuendesha kilimo chenye tija kwa kukumbatia mfumo wa mashamba ya ‘ghorofa’ ambayo kwanza hudumisha ubora wa mchanga.
Aidha mkulima anaweza kuboresha kilimo kwa kuweka aina maalum ya sensa kwenye mfumo huu, ili kuchanganua ubora wa udongo, hali ya hewa na kiwango cha unyevu kwa ajili ya ukuaji bora wa mimea.
Kupitia mfumo huo, mkulima anaweza kudhibiti wadudu ambao hushambulia mazao yanapokuwa shambani.
“Mashamba ya ghorofa huzalisha chakula chenye ubora wa hali ya juu na kwa wingi hivyo basi mkulima anaweza kuwekeza katika shughuli hii akilenga kuendesha kilimo kibiashara,” asema.
Anaeleza kuwa kufikia sasa, Greenhouse Bomba Farms wameanzisha harakati ya kuwafikia vijana, akina mama na wale wenye ulemavu akiamini ni kundi la watu ambao wamesahaulika.
Kwa ushirikiano na Jamii Action Centre, wanatumia mitandao ya kijamii kama vile Whatsapp, X, Facebook na Instagram kupokezana na kubadilishana mawazo kuhusu kilimo toshelevu.
Kupitia majukwa haya pia wanaelimishana namna ya kuendesha kilimo cha kutumia maji kidogo cha ‘zai pits’ ambacho hushirikisha uchimbaji wa mashimo ya mviringo kandokando ya mimea ambayo hujaziwa maji na mchanga wenye rutuba.
Pia hayapotezi maji kwa urahisi.
Kulingana na Juma, aina hii ya kilimo inasaidia kuhakikisha upatikanaji wa vyakula vya asili, mboga na matunda yenye virutubisho vingi ambavyo ni muhimu kwa afya ya binadamu.
“Kwa kuwa na upatikanaji wa chakula bora na chenye virutubisho, jamii hupata afya bora na kuepuka magonjwa yanayoweza kuzuilika kama vile utapiamlo na upungufu wa damu.”
Pia mazao ya kilimo kama mboga na matunda ni muhimu katika kuimarisha kinga mwilini.
Kilimo cha mashamba ya ghorofa mijini huchochea biashara na shughuli za usafirishaji wa bidhaa kutoka mashambani hadi masokoni au nje ya nchi.
Vilevile hupunguza gharama ya usafirishaji wa mazao ghafi kutoka maeneo ya vijijini hadi mijini.
Hii husaidia kukuza biashara za mazao ya kilimo kama vile mboga, matunda, na nafaka, hivyo kutoa ajira kwa wauzaji, wasafirishaji na wafanyabiashara.
Kadhalika, uzalishaji mkubwa wa mazao huchangia katika biashara za kimataifa kupitia mauzo ya nje.