Sakaja ‘akabidhi’ Ruto majukumu ya jiji licha ya kupinga NMS awali
GAVANA wa Nairobi Johnson Sakaja, ambaye aliwahi kujisawiri kama mtetezi wa ugatuzi na kupinga iliyokuwa Huduma ya Jiji la Nairobi (NMS), sasa anakabiliwa na mtihani mkubwa baada ya kuthibitisha kuwa utawala wake unashirikiana na serikali ya kitaifa katika utoaji huduma jijini.
Ushirikiano huo unahusu ukusanyaji taka, ujenzi na ukarabati wa barabara, huduma za maji taka na majukumu mengine ya msingi ya kaunti.
Hii ni licha ya msimamo wake wa awali kwamba, hangerejea kwa mpango wa NMS wala kuhamishwa kwa majukumu ya ugatuzi hadi serikali kuu.
Kwa kipindi cha miaka miwili iliyopita, mashirika ya kitaifa yameonekana wazi yakitekeleza miradi ya barabara na usafi jijini, huku Huduma ya Vijana kwa Taifa (NYS) wakihusika.
Akizungumza katika hotuba yake ya Hali ya Kaunti Jumatano, Sakaja alisisitiza kuwa mazungumzo yake na Rais William Ruto ni ya ushirikiano uliopangwa, si makabidhiano ya kikatiba.
“Ni ushirikiano, si uhamisho wa majukumu,” alisema, akiongeza kuwa jiji kuu haliwezi kumudu kukosa mpangilio wa huduma.
Alikumbusha athari za NMS akidai mpango huo uliacha kaunti na deni za Sh16 bilioni pamoja na changamoto za kiutawala.
“Hatutaruhusu uhamisho wa majukumu ya kaunti tena” alisisitiza.