Zámba Heritage: Wito viongozi wa Afrika washirikiane kulinda misitu
KONGAMANO la Zámba Heritage lililofanyika jijini Nairobi kuanzia Februari 10 hadi Februari 12 liliwaleta pamoja viongozi kutoka nchi mbalimbali, wataalamu wa mazingira, wanaharakati na sekta binafsi kujadili mustakabali wa misitu barani Afrika.
Mkutano huo umeangazia umuhimu wa kutekeleza baadhi ya sera ambazo tayari zipo ili kulinda misitu.
Chini ya kaulimbiu ya kuimarisha urithi wa misitu kwa vizazi vya sasa na vijavyo, washiriki wamejadili nafasi ya misitu katika kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi na kuboresha maisha ya jamii zinazoishi karibu na misitu.
Akizungumza wakati wa kongamano hilo, mmoja wa maafisa wakuu wa sekta ya misitu barani Afrika alisema kuwa wakati umefika kwa mataifa ya Afrika kuweka mikakati thabiti ya usimamizi wa misitu bila kuathiri maendeleo ya kiuchumi kama vile kilimo, uchimbaji madini na miradi ya miundombinu.
Kulingana na Annah Agasha, Naibu Mkurugenzi wa kikanda baraza la usimamizi wa misitu barani Afrika, kuna haja vijana washirikishwe kwa kupewa elimu ya kutosha kuhusu umuhimu wa kuhifadhi msitu kwani ndio viongozi wa kesho.
“Vijana wanafaa kuwa katika mstari wa mbele katika mpango huu kwani ndio viongozi wetu wa kesho,” alisema Bi Agasha.
Aidha, suala la fedha za tabianchi na biashara ya kaboni limepewa uzito, huku nchi zikihimizwa kutumia fursa za masoko ya kaboni kufadhili miradi ya uhifadhi wa misitu.
Hata hivyo, wadau walisisitiza kuwa jamii za wenyeji lazima zihusishwe kikamilifu ili kuepusha migogoro na kuhakikisha manufaa yanawafikia moja kwa moja.
Kwa upande wa Kenya, mjadala umejikita katika juhudi kurejesha na kuhifadhi maeneo yaliyoharibiwa kama vile Mau na Aberdare.
Wataalamu wanasema mafanikio yatategemea uwazi, ushirikishwaji wa wananchi na utekelezaji madhubuti wa sera.
Kongamano hilo linatarajiwa kutoa mwongozo wa hatua za pamoja zitakazochukuliwa na mataifa ya Afrika katika kulinda rasilimali za misitu, ambazo ni nguzo muhimu katika mapambano dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.