Msongamano wazidi bandarini mashirika husika yakilaumiana
MSONGAMANO mkubwa unaendelea kushuhudiwa katika Bandari ya Mombasa huku mashirika husika yakirushiana lawama.
Waziri wa Barabara na Uchukuzi Davis Chirchir ameonya kuwa wakuu wa mashirika ya serikali watakaoshindwa kutekeleza maagizo yaliyowekwa ili kupunguza msongamano huo watafutwa kazi.
Bw Chirchir, aliyekuwa bandarini Mombasa kujadili suluhu za kupunguza zaidi ya meli 20 zinazongoja kuhudumiwa pamoja na zaidi ya makontena 500 matupu ambayo hayajarejeshwa, alisema jukumu lake si kusimamia shughuli za kila siku.
“Iwapo niko hapa nikijadili shughuli za uendeshaji, basi kuna mtu hafanyi kile anachopaswa kufanya. Kuna tatizo la uratibu miongoni mwa mashirika husika ya serikali,” alisema Waziri huyo.
Katika miezi ya hivi karibuni, mashirika mbalimbali yanayoshughulikia mizigo, ikiwemo Mamlaka ya Bandari Kenya (KPA), Mamlaka ya Ukusanyaji Ushuru Kenya (KRA) na ya usafirishaji, yamekuwa yakirushiana lawama kuhusu ongezeko la msongamano bandarini.
Katika mkutano huo, Waziri aliidhinisha KPA kununua vifaa vya ziada vya kushughulikia mizigo ili kuharakisha shughuli hizo, akibainisha kuwa kuna upungufu wa zaidi ya trekta 80 za kubeba makontena.
Kama suluhu ya muda mfupi, serikali imerejesha usafirishaji wa lazima wa mizigo kwa njia ya reli kutoka Bandari ya Mombasa kuelekea mataifa yasiyo na bandari, hatua inayolenga kupunguza msongamano huku bandari ikiwa imeathiriwa.
Hata hivyo, hatua hiyo imezua upinzani mkali kutoka kwa wasafirishaji, wakisema agizo kama hilo lilitangazwa kuwa kinyume cha sheria na Mahakama Kuu mwaka 2020.
Tangu Ijumaa iliyopita, malori yanayochukua mizigo bandarini yamesimamishwa kufuatia uboreshaji wa mfumo wa KRA ambao haujarejeshwa kikamilifu wiki moja baadaye.
Hali hiyo imesababisha msongamano mkubwa wa magari, na kulazimu KRA kuelekeza mizigo yote inayoelekea Uganda, Sudan Kusini, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo na Rwanda kupewa kipaumbele kusafirishwa hadi Kituo cha Kontena cha Ndani cha Naivasha (ICD).
Mnamo Jumanne, Kamishna Mkuu wa KRA Humphrey Wattanga alitangaza kuwa Naivasha ICD itapewa kipaumbele kwa mizigo ya kuelekea nchi jirani kutokana na ongezeko la mizigo bandarini Mombasa.
Hata hivyo, wadau mbalimbali wa bandari, wakiwemo mawakala wa forodha na Chama cha Wasafirishaji Kenya (KTA), wamepinga vikali pendekezo la kufanya Naivasha ICD kuwa njia ya lazima ya kupitisha mizigo.
Mwenyekiti wa KTA Newton Wang’oo alisema kituo hicho hakina msingi wa kibiashara kuhalalisha uamuzi huo, na kwamba agizo hilo litakiuka haki ya wamiliki wa mzigo kuchagua mahali pa kuondolea mzigo na njia ya usafirishaji.
“Msongamano wa sasa umetokana na upangaji duni, matatizo ya ratiba za meli na changamoto za kuondoa makontena matupu. Meli zinaondoka bila kujazwa kikamilifu kwa sababu haziwezi kusubiri kupakiwa makontena matupu. Haya hayawezi kutatuliwa kwa kulazimisha mizigo kuelekezwa Naivasha,” alisema Bw Wang’oo.
Mnamo Novemba 2020, Mahakama Kuu ilibatilisha agizo la KPA na KRA lililowataka waagizaji wote kusafirisha mizigo kutoka Mombasa hadi Nairobi kwa reli ya SGR, ikisema halikufuata misingi ya ushirikishaji wa umma.
Katika wiki iliyopita, malori yaliyokuwa yakielekea bandari yalisimamishwa, hali iliyosababisha msongamano wa magari kwa zaidi ya kilomita tatu.
Wakati huohuo, shughuli bandarini zimeathiriwa na ukarabati na utengenezaji wa mfumo wa KRA wa Integrated Customs Management System (iCMS), unaotumika kuondoa mizigo ya kuingia na kutoka nchini.
KRA ilitangaza kuwa mfumo huo ungefungwa kwa saa 36 kuanzia Jumamosi, Februari 7, 2026 saa 12 jioni hadi Jumatatu, Februari 9, 2026 saa kumi na mbili asubuhi, ili kufanyiwa ukarabati mkubwa.
“Tungependa kufahamisha mashirika husika ya serikali, waagizaji, wasafirishaji, mawakala wa forodha, kampuni za meli na umma kwa ujumla kuhusu utengenezaji uliopangwa wa mfumo wa iCMS,” ilisema KRA.