Je, Sifuna atanaswa na ndoana ya Muungano wa Upinzani?
MUUNGANO wa Upinzani umerushia ndoano waasi wa chama cha ODM baada ya seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kuvuliwa wadhifa wa katibu mkuu na dalili zikiwa wazi kwamba huenda akatimuliwa katika chama hicho cha chungwa.
Aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua amedokeza uwezekano wa kuundwa kwa ushirikiano kati ya Muungano wa Upinzani na mrengo wa waasi ndani ya chama cha Orange Democratic Movement (ODM) unaohusishwa na Seneta Sifuna.
Akizungumza katika mahojiano na K24 TV pamoja na vituo kadhaa vya redio vya jamii ya Maa Jumatano, Februari 10, 2026, kiongozi wa chama cha Democracy for Citizens Party (DCP) alitaja mrengo huo wa ODM katika mikakati ya Muungano wa Upinzani.
Alisema iwapo kundi hilo litamsimamisha mgombea urais mwenye nguvu wa kumenyana na Rais William Ruto, kama vile Gavana wa Siaya James Orengo, basi vinara wa sasa wa upinzani wanaowania kiti cha urais wako tayari kuweka kando azma zao na kumuunga mkono mgombea huyo.
Gachagua alirejelea mrengo huo kama “ODM B” katika harakati zao za kumwondoa Rais Ruto mamlakani kupitia uchaguzi wa 2027.
Aidha, alimtaja Seneta wa Busia Okiya Omtatah kama mmoja wa wanaoweza kuwania urais kupitia muungano huo mpana wa upinzani, akisema viongozi wa upinzani wako tayari pia kumpisha iwapo ataonekana kuwa na umaarufu na ushawishi wa kutosha kupeperusha bendera ya urais.
“Kama hawa watu wa ODM B watatoa mtu aje, kama ni Omtatah, pia aje, tukae chini, tuulizane nani kati yetu ako na umarufu wa kutosha wa kusukuma huyu mtu aende nyumbani. Tutasikizana,” alisema Gachagua.
Mrengo unaomuunga mkono Sifuna, ambao sasa unajulikana kama ODM Linda Wananchi, umekuwa ukizuru maeneo mbalimbali nchini kufanya mikutano ya kisiasa.
Wanatarajiwa kufanya mkutano mkubwa leo katika miji kadhaa ya Kajiado baada ya uliofaulu sana Kaunti ya Busia.
Kundi hilo lilijitenga na mrengo unaoongozwa na Oburu Odinga kufuatia pendekezo la chama kuanza mazungumzo ya kuungana na chama tawala cha United Democratic Alliance (UDA).
Mrengo huo umekosoa vikali uongozi wa juu wa ODM kwa kile wanachodai ni kushindwa kusimamisha mgombea urais na badala yake kumuunga mkono Rais Ruto kuwania muhula wa pili.
Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, ambaye ni miongoni mwa waasi hao, pia ameonyesha kutoridhishwa na mwelekeo wa chama, akisema kuwa katika kipindi cha uongozi wa kisiasa wa Raila Odinga, ODM haikuwa ikitafuta miungano bali vyama vingine ndivyo vilikuwa vikijiunga nacho kuunda ushirikiano.
Hata hivyo, baadhi ya wanachama wa mrengo unaoongozwa na Oburu wamekataa vikali mazungumzo na chama cha DCP cha Gachagua wakidai kuwa vyama hivyo viwili havina misingi wala maadili ya kisiasa yanayofanana.
Haya yanajiri wakati vinara wa Muungano wa Upinzani akiwemo kiongozi wa Wiper Kalonzo Musyoka, kiongozi wa PLP Martha Karua, kiongozi wa DAP-K Eugene Wamalwa, kiongozi wa Democratic Party JB Muturi, Fred Matiang’i wa Jubilee na Gachagua mwenyewe, wote wakikutana Naivasha kuweka mikakati ya kumenyana na Ruto katika uchaguzi mkuu wa 2027.
Democratic Action Party–Kenya (DAP-K), kinachoongozwa na aliyekuwa na Wamalwa, kimetangaza wazi nia yake ya kuwashawishi Bw Sifuna na viongozi wengine wa ODM wanaochukuliwa kuwa waasi kujiunga nacho.
Akizungumza Ijumaa wakati wa kupandishwa hadhi kwa Soko la Kiminini kuwa mji mdogo katika Kaunti ya Trans-Nzoia, Bw Wamalwa alisema chama chake kimeamua kuwakaribisha viongozi wanaohisi kutengwa ndani ya ODM.
“Tumeamua kuwaalika ndugu zetu wanaopigwa vita ODM kwa lengo la kuwakaribisha wajiunge na chama chetu,” alisema Bw Wamalwa.Aliwataja mahsusi Bw Sifuna na Mbunge wa Saboti Caleb Amisi kama viongozi ambao DAP-K iko tayari kuwakaribisha.
Vinara hao wamekuwa wakiahidi wafuasi wao kwamba wako tayari kuweka kando azma za kibinafsi na kuunga mkono mmoja wao kushindana na Rais Ruto katika uchaguzi mkuu ujao.