Siasa

Oburu sasa aonywa akome kutamani kiti cha Prof Kindiki

Na DAVID MUCHUI February 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WANASIASA wa chama tawala kutoka eneo la Mlima Kenya wamekionya chama Orange Democratic Movement (ODM) dhidi ya kulenga wadhifa wa Naibu Rais, wakisema kuwa hauko wazi katika uongozi wa nchi.
Kauli hizo zinafuatia matamshi ya hivi majuzi ya kiongozi wa ODM Oburu Oginga, aliyesema chama hicho kina nia ya kuhakikisha kitapata wadhifa wa Naibu Rais kupitia makubaliano ya muungano wa kisiasa mwaka 2027.
Wakizungumza Ijumaa katika mikutano ya uwezeshaji mjini Meru, wabunge wanaomuunga mkono Rais William Ruto na naibu wake Kithure Kindiki walisema kuwa wadhifa wa Naibu Rais hauwezi kujadiliwa, wakiahidi kuulinda kwa hali na mali.
Gavana wa Tharaka Nithi Muthomi Njuki aliwaonya viongozi wa ODM akisema kiti hicho tayari kinashikiliwa na kiongozi mwenye uwezo.
Gavana Njuki alisisitiza kuwa wadhifa wa Naibu Rais haupaswi kuwa ajenda katika mazungumzo ya muungano kati ya UDA na ODM.
“Hakuna sababu ya msingi ya wadhifa wa Prof Kindiki uwe ajenda katika mazungumzo. ODM inapaswa kushughulika na kurekebisha mgawanyiko ndani ya chama chao. Ikiwa madai hayo yataendelea, basi chama tawala cha UDA kinaweza ‘kumkabidhi’ Kindiki kwa ODM lakini abaki kuwa Naibu Rais,” alisema Njuki.
Wakiongozwa na Mbunge wa Laikipia Mashariki Mwangi Kiunjuri, wabunge walisema matamshi ya kiongozi wa ODM ni tishio la moja kwa moja kwa washirika wa Rais Ruto katika eneo la Mlima Kenya.
Kiunjuri aliandamana na wabunge Moses Kirima (Imenti Kati), Johnpaul Mwirigi (Igembe Kusini), John Mutunga (Tigania Magharibi), Mugambi Rindikiri (Buuri) na Dorothy Muthoni (Mteule).
“Hakuna mjadala wowote kuhusu wadhifa waNaibu Rais nchini Kenya. Tunawahimiza marafiki zetu wa ODM washughulikie mkanganyiko ndani ya chama chao. Wakati watapanga mambo yao, sisi tutakuwa tunaimarisha nafasi yetu serikalini. Tutalinda kiti hicho kwa gharama yoyote,” alisema Kiunjuri.
Aliongeza: “ODM inapaswa kuonywa kwamba ofisi ya Naibu Rais kwa sasa ni kama mwanamke aliye kwenye ndoa halali. Ukijaribu kumtongoza, ni kwa hatari yako.”
Alisema washirika wa Prof Kindiki sasa wanalenga kuongeza uungwaji mkono wa Rais Ruto katika eneo hilo ili kuzuia ushawishi wa ODM.
“Tishio kubwa la kisiasa kwa eneo la Mlima Kenya ni sisi wenyewe iwapo hatutapiga kura kwa wingi kuonyesha kwamba tunastahili wadhifa wa Naibu Rais. Rais Ruto akishinda, Prof Kindiki anashinda. Hilo ndilo tunapaswa kulinda,” alisema Mbunge huyo wa Laikipia Mashariki.
Mbunge wa Buuri Mugambi Rindikiri alisema ODM inapaswa kujiepusha na masuala ya urais mwaka 2027.
“Ukweli ni kwamba Prof Kindiki atasalia kuwa Naibu Rais mwaka 2027 na kuendelea. Kiti hicho kinalindwa na kura tulizompa Rais Ruto mwaka 2022,” alisema Rindikiri.
Mbunge wa Imenti Kati Moses Kirima alisema kuwa ingawa vyama zaidi vya siasa vinakaribishwa kufanya kazi na serikali, vinapaswa kuheshimu mipaka iliyowekwa.
“Haijawahi kusikika kwa mgeni kumtimua mwenyeji wake kutoka kwenye kiti chake. Mgeni mwema huridhika na kiti anachopewa,” alisema Kirima.
Alihoji kwa nini ODM inalenga wadhifa wa Prof Kindiki ilhali haikuchangia kura kwa Rais.
“Prof Kithure Kindiki si Naibu Rais kwa bahati. Alifika hapo kwa sababu tulimpigia kura Rais William Ruto kwa wingi mwaka 2022,” alisema mbunge huyo.
Mbunge wa Tigania Magharibi John Mutunga alisema matamshi ya kiongozi wa ODM ni mwamko kwa eneo la Mlima Kenya kuelekea Uchaguzi Mkuu wa 2027.
“Ni lazima tujiandae kukabiliana na ODM kwa kuandikisha wapiga kura wengi iwezekanavyo. Lazima tulinde kiti cha Naibu Rais kwa kura nyingi mwaka 2027. Huu ni mchuano wa kufa au kupona,” alisema Mutunga.
Mbunge Mteule Dorothy Muthoni alisema atawahamasisha wanawake wa Meru kulinda wadhifa Naibu Rais dhidi ya ODM.
“Prof Kindiki si tu mwana wetu bali pia ni mchapa kazi mahiri na msimamizi wa ajenda ya uchumi wa chini kwenda juu. Eneo la Mlima Kenya
Wanasiasa hao waliapa kulinda eneo hilo dhidi ya kile walichokitaja kuwa mashambulizi ya upinzani.