Wazee Kajiado waangalia matumbo ya mbuzi na kutangaza mvua inakuja
WAZEE na wataalamu wa Idara ya Utabiri wa Hali ya Hewa wametabiri kuwa baadhi ya sehemu za Kaunti ya Kajiado zitapokea mvua kati ya Machi-Aprili 2026.
Tangazo hilo limewapa wakazi wengi matumaini ikizingatiwa kaunti hiyo kwa sasa inaendelea kukeketwa na ukame.
Mamlaka ya Kitaifa ya Kupambana na Ukame (NDMA) imeorodhesha kaunti hiyo kama inayoandamwa na ukame na kusema zaidi ya nyumba 64,300 zinakabiliwa na ukame.
Takwimu ya hivi majuzi kutoka NDMA inaonyesha kuwa zaidi ya Wakenya milioni 2.1 waliathiriwa na ukame mnamo Januari na idadi hiyo imepanda hadi milioni 3.3 mnamo Februari.
Kaunti 23 kame zimeathirika na ukame huo na serikali imetenga Sh10 bilioni kuokoa hali.
Wafugaji kutoka maeneo mbalimbali ya Kajiado wamehama na mifugo yao hadi kaunti jirani.
Mnamo Alhamisi, wazee wa Maa walifanya tambiko mjini Kajiado ili kuleta mvua.
Tambiko hilo lilihusisha kuchinjwa kwa mbuzi kisha matumbo yake yakaangaliwa kutabiri hali ya hewa.
Mzee Moses Ole Nkina, 70, aliongoza tambiko hilo lililodumu kwa dakika 30 kabla ya wazee hao kutangaza kuwa mvua inakuja siyo Umasaini tu bali pia sehemu nyingine za nchi.
Walibaini kuwa damu kwa kiasi cha chini, ilitiririka katika sehemu ya mishipa polepole, hilo likiashiria mvua chache maeneo ya kusini.
“Damu ilienea sana sehemu nyingine ya mishipa na hilo linaonyesha mvua zaidi ya kiwango cha wastani maeneo ya Kaunti ya Kajiado na mengine nchini,” akasema Mzee Nkinai lakini akasema hajui ni lini mvua itaanza.
Naye Mkurugenzi wa Idara ya Utabiri ya Hali ya Hewa Kajiado Benson Lubanga alisema mtazamo wa kisayansi unalandana na njia za kitamaduni.
Kwa mujibu wa Bw Lubanga, maeneo ya kaskazini na magharibi mwa nchi yanatarajiwa kupokea mvua inayozidi kiwango cha wastani.
“Kaunti hii itapokea mvua kwa kiwango cha wastani huku mengine yakipokea mvua zaidi ya wastani. Tunatarajia wafugaji wazingatie hili,” akasema Bw Lubanga.
Kamishina wa Kaunti ya Kajiado Michael Yator alisema kuwa serikali inachukua hatua za dharura ili kuhakikisha kuwa hakuna anayekufa njaa kutokana na ukame huo.