Habari za Kitaifa

Njaa: Maelfu Mandera, Marsabit wachungulia kaburi

Na MANASE OTSIALO February 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

KAUNTI za Mandera na Marsabit ndizo zinakabiliwa na hatari kuu zaidi ya kudhuriwa na ukame, hali inayohatarisha maisha ya wakazi na mifugo kutokana na ukosefu wa maji na malisho kote katika eneo hilo.

Ardhi imekauka na kupasukapasuka, maji yameadimika, huku joto kali likisababisha vichaka kudidimia na mifugo kufa.

Kamishina wa Mandera James Chacha anasema hali inazidi kuzorota kote katika kaunti hiyo huku maeneo yaliyoathirika zaidi yakijumuisha Mandera Kaskazini, Kati, Lafey na Mandera Magharibi.

Watu wapatao 300,000 wameathiriwa na idadi inazidi kupanda huku mvua ikikosa kunyesha na malisho kutoweka.

“Kiangazi kinatisha. Kuna haja ya mikakati endelevu ili kuokoa maisha ya binadamu na mifugo,” akasema Bw Chacha.

Serikali ya kaunti hiyo inavisambazia maji takriban vituo 299 lakini mahitaji yanazidi kwa mbali rasilimali zinazopatikana, na kuacha familia zikizidi kuathirika kwa sababu mifugo ikitembea mwendo mrefu, viwango vya maziwa vinadorora na familia zinakosa uwezo wa ununuzi.

Ili kupata maji, wanakijiji ni sharti wachange Sh25,000 kukodisha lori la lita 10,000, kiasi ambacho ni muhali kwa familia nyingi ambazo tayari zimepokonywa utajiri wazo wa mifugo.

Vijiji kadhaa vimeathirika ikiwemo vituo vya mpakani vilivyoonekana awali kama mikondo ya kujifaidi ambavyo sasa vimegeuka njia za kukatisha tamaa.

Katika kijiji cha Awara, makali ya kiangazi yamesababisha mimea na malisho kukauka.

Juhudi za kuweka mifugo hai zimekuwa ghali huku baadhi ya wakazi wakilazimika kusafiri mara moja kwa wiki mjini Rhamu, karibu kilomita 10, kununua malisho ya mifugo kwa sababu mimea haikui tena Awara.

Hali hiyo ya kusikitisha imegeuza masoko kuwa mahali pa ukandamizaji.