Sifuna, kijana wakili anayepitia mawimbi ya siasa: Ijue historia yake
SENETA wa Nairobi Edwin Watenya Sifuna anaendelea kujijenga kama mmoja wa wanasiasa shupavu na wakili anayejua kuogelea mawimbi ya siasa za Kenya bila kuyumba.
Sifuna alizaliwa Mei 22, 1982 katika Hospitali ya St Mary’s, Mumias, Kaunti ya Kakamega. Baba yake alikuwa mtumishi wa umma katika iliyokuwa Halmashauri ya Manisipaa, huku mamake akiwa mwalimu wa shule ya msingi.
Ami yake, Lawrence Sifuna alikuwa mwanasiasa machachari aliyewakilisha eneo bunge la Bumala.
Sifuna alianza masomo yake katika Shule ya Msingi ya Kakamega Township kabla ya kujiunga na Shule ya Upili ya Musingu alikofanya mtihani wa KCSE.
Baadaye alisomea Shahada ya Sheria (LLB) katika Chuo Kikuu cha Nairobi na kuhitimu mwaka 2006. Aliendelea na Stashahada ya Uzamili katika Shule ya Sheria Kenya mwaka 2007, kisha kufanya mafunzo ya uwakili katika kampuni ya Kairu & McCourt Advocates. Aliapishwa rasmi kama wakili wa Mahakama Kuu mwaka 2008.
Safari yake ya kisiasa ilianza kuonekana wazi mwaka 2013 alipojiunga na muungano wa CORD kama mjumbe wa kamati ya kiufundi na ushauri.
Baadaye aliendelea na jukumu hilo ndani ya muungano wa NASA. Mwaka 2017 alijaribu bahati yake kuwania ubunge wa Kanduyi kupitia tiketi ya ODM lakini hakufaulu katika kura za mchujo.
Hata hivyo, ODM ilimteua kuwania kiti cha Useneta wa Nairobi katika uchaguzi mkuu wa 2017. Ingawa alishindwa na Johnson Sakaja, alijizolea zaidi ya kura 674,000, akithibitisha kuwa alikuwa ameanza kujijengea jina katika siasa za jiji kuu.
Mwaka 2018 aliteuliwa kuwa Katibu Mkuu wa ODM kuchukua nafasi ya Ababu Namwamba. Katika nafasi hiyo, alijitokeza kama msemaji mkali wa chama na mtetezi wa misingi ya demokrasia ya vyama vingi. Mwaka 2019 alichaguliwa kuwa makamu mwenyekiti wa Centre for Multiparty Democracy (CMD), akiongeza sifa zake katika siasa za kitaifa.
Katika uchaguzi mkuu wa 2022, Sifuna alirejea tena kuwania Useneta wa Nairobi na kushinda kwa kura 716,876. Tangu wakati huo, amekuwa akihudumu kama Seneta wa Nairobi na pia Naibu kiongozi wa Wachache katika Seneti.
“Sifuna si mwanasiasa wa kawaida. Ni wakili aliyekuzwa na maadili ya haki na usawa tangu utotoni, misingi ambayo ilimwelekeza kusomea Shahada ya Sheria na baadaye kuingia katika medani ya siasa kwa lengo la kupigania Wakenya wa kawaidam,” anasema katika tovuti yake.