Habari za Kitaifa

Wahuni mikutanoni: Tutasaidia Gachagua tu iwapo ataandikisha taarifa, Polisi wasema

Na MWANGI MUIRURI February 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

TUME ya Huduma kwa Polisi (NPS) sasa inamtaka Kiongozi wa DCP Rigathi Gachagua aandikishe taarifa rasmi kuhusu tukio la Januari 25 ambapo polisi na watu wanaoshukiwa kuwa wahuni, waliwavamia waumini katika Kanisa la Witima, eneobunge la Othaya, Kaunti ya Nyeri.

Video zilizosambaa mitandaoni zilionyesha waliotekeleza uvamizi huo wakifyatua risasi, kurusha mawe na pamoja na vitoza machozi ndani ya kanisa.

Polisi waliokuwa wakipiga doria walionekana wakiwaunga mkono wahuni hao.

Kwenye taarifa iliyotolewa jana na kutiwa saini na Msemaji wa Polisi Muchiri Nyagah, NPS alisema kasi na ufanisi wa uchunguzi huo unategemea Bw Gachagua kuandikisha taarifa.

“Inategemea kuandikisha taarifa rasmi, mashahidi kueleza yaliyotokea kwa kina kisha kushirikiana kwa walalamishi na umma,” akasema Bw Nyagah.

Alisema baada ya kupokea ripoti ya uhalifu kutokea, polisi walianzisha uchunguzi kwa kufuata sheria.

Bw Nyagah alisema kuwa kwa sasa kinachofahamika ni maelezo ambayo yapo mitandaoni lakini akasema uchunguzi zaidi wa kina unahitajika kupitia ushahidi kutoka kwa umma.

“Polisi wameandikisha taarifa na pia video ambayo ilikuwa imesambazwa mitandaoni imeangaliwa huku waliohusika wakitambuliwa. NPS inaomba yeyote mwenye habari au maelezo muhimu ajitokeze na kuwasaidia polisi wanaochunguza kisa hiki,” akasema.