Habari za Kitaifa

Juhudi mpya za kupatanisha Uhuruto zaendelea

Na JUSTUS WANGA February 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

IMEBAINIKA kuwa uhasama kati ya Rais William Ruto na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta ulichipuka wiki jana katika kikao cha Umoja wa Afrika (AU), wawili hao wakilaumiana katika mkutano wa faragha ambao uliandaliwa na Waziri Mkuu wa Ethiopia Abiy Ahmed kuwapatanisha.

Wawili hao walikuwa katika mkutano ambao uliandaliwa kusaidia kurejesha amani Mashariki mwa Jamuhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC).

Uhasama kati ya wawili kwenye mkutano huo wa Jumapili ulithibitishwa na baadhi ya wasaidizi wao, washirika na waliokuwa kwenye mkutano huo ambao walisema ulipaka tope sifa za nchi machoni pa ulimwengu.

Picha iliyosambaa mtandaoni ikionyesha Bw Ahmed akiwa katikati ya Rais Ruto na Bw Kenyatta ilichapishwa mitandaoni na upande wa rais huyo mstaafu.

Hata hivyo, mrengo wa Rais Ruto haukutundika picha hiyo mtandaoni na kuibua maswali kuhusu kiini cha hatua yao.

Marais wanachama wa AU walizua maswali kuhusu jinsi mchakato wa kupatikana kwa amani mashariki mwa DRC umekosa kupiga hatua na ikabainika ni kwa sababu ya uhasama kati ya Bw Kenyatta na Rais Ruto.

Huku Rais akihusika na juhudi za moja kwa moja za amani kwa kutuma vikosi vya jeshi mashariki mwa DRC, Bw Kenyatta yupo kwenye jopo la AU pamoja na miungano ya kiuchumi ya EAC na SADC ambayo ina jukumu la kushiriki upatanishi Ituri, Kivu Kaskazini na Kusini ambako vita vimechacha.

Bw Kenyatta anastahili kushauriana na Rais Ruto kwa kumfahamisha kuhusu hatua zilizopigwa na changamoto zilizopo katika mchakato wa kupatikana kwa amani mashariki mwa DRC.

Hata hivyo, ilibainika uhasama kati ya wawili hao umerejesha nyuma au kukwamisha juhudi za amani huku raia wa mashariki mwa DRC wakiumia.

Hapo ndipo Bw Ahmed alianza mchakato wa kuwapatanisha wawili hao ili kuhakikisha mpango wa kurejesha amani DRC unafaulu. Tofauti hizo kali zilichipuka AU wiki tatu tu baada ya Muhoho Kenyatta, nduguye Bw Kenyatta, kuandaa kikao na Rais Ruto katika ikulu ya Nairobi.

Katika siasa za hapa nchini, Bw Kenyatta ameonekana kuunga azma ya Kinara wa Wiper Kalonzo Musyoka, kufufua Jubilee na kuidhinisha uongozi wa aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiangí.

Uongozi wa Rais Ruto nao umekuwa ukiandamwa na changamoto kadhaa kutokana na sera hasi ambazo zinadaiwa kuwaumiza raia na mnamo 2024 ilitikiswa na maandamano ya Gen Z nchini.

Bw Kenyatta kuendelea ‘kukataa’ kustaafu na kuendelea kujihusisha na siasa, kunaonekana kumkera Rais Ruto anayesaka muhula wa pili mnamo 2027.

“Rais Ruto alimkabili Bw Kenyatta na ushahidi lakini rais mstaafu akakanusha kuwa alikuwa akipiga vita utawala wa Kenya Kwanza. Hata hivyo, alilalamika kuwa hajakuwa akiheshimiwa na kushughulikiwa vyema kama rais mstaafu,” duru zilizohudhuria mkutano zikaarifu.

Rais Ruto alimwambia Bw Abiy kuwa amejaribu kupatanishwa na Bw Kenyatta lakini mchakato huo haujafua dafu.

“Hata alitaja ziara yake nyumbani kwa Bw Kenyatta Ichaweri mnamo 2024 na juhudi nyingine kupitia jamaa zake,” duru hizo zikaarifu.

Munyori Buku, Mkuu wa mawasiliano Ikulu alisema hana ufahamu wa yaliyojiri kwenye mkutano huo.

“Sijajua kama kulikuwa na mkutano wa upatanishi lakini ni kweli Rais Ruto na Rais Mstaafu Uhuru Kenyatta walikutana na Waziri Mkuu Abiy. Sina maelezo kuhusu yaliyojiri kwa sababu ulikuwa mkutano wa faragha,” akasema Bw Buku.

Msemaji wa Bw Kenyatta, Kanze Dena naye alishangaza na madai kuwa kulikuwa na juhudi za kuwapatanisha wawili hao kutokana na uhasama kati yao.

“Kwani wasisalimiane kiasi kwamba wakifanya hivyo mnachanganua. Acheni hizo, sasa picha imekuwa hoja ya kuchanganuliwa?” akasema Bi Dena.