Karua abandikwa jina ‘mgeni asiyetakikana’ na serikali ya Uganda, afurushwa
KIONGOZI wa chama cha PLP, Bi Martha Karua jana alisema kuwa Uganda imerejelea uongozi wa kidikteta kama enzi za Rais Idi Amin Dada baada ya kuzuiliwa katika uwanja wa ndege wa Entebbes na kufurushwa nchini humo.
Bi Karua alizuiliwa katika uwanja huo kisha akarejeshwa Kenya. Waziri huyo wa zamani wa Katiba na Sheria alikuwa amesafiri Uganda kwa ndege ya Kenya Airways pamoja na Rais wa Chama cha Mawakili nchini (LSK) Charles Kanjama kuhudhuria kikao cha korti kuhusu kesi ya Kiongozi wa Upinzani Uganda Kizza Besigye.
Bw Besigye amekuwa akizuiliwa baada ya kushtakiwa kwa kosa la uhaini na mawakili wake wakiongozwa na Bi Karua na jana ilikuwa siku ya kusikizwa kwa kesi ambapo anataka awaachiliwe kwa dhamana.
Bi Karua alikuwa ametua katika uwanja wa Entebbe kujiunga na mawakili wa Bw Besigye akiwemo Wakili Erias Lukwago.
Bw Lukwago mwenyewe alishtakiwa kwa makosa ya uhaini wiki jana na kesi yake ya kuachiliwa kwa dhamana ilikuwa isikizwe pia jana.
“Uganda imerejea katika uongozi kama wa Amin Dada ambapo jeshi ndilo linachukua usukani kutoka kwa polisi,” akasema Bi Karua baada ya kutua katika uwanja wa ndege wa JKIA jana jioni.
Serikali ya Uganda haikutoa sababu za kumzuia Bi Karua japo Bw Kanjama aliruhusiwa kuingia.
“Mbona iwe marufuku kwangu kusafiri nchi ya ukanda wa Jumuiya ya Afrika Mashariki ilhali nina pasipoti ya Afrika Mashariki na kuna Jumuiya ya Afrika Mashariki? Ama jumuiya hii ni klabu ya viongozi?” akauliza Bi Karua.
Bw Kanjama mwenyewe alishangazwa na hatua hiyo akisema wote ni mawakili na walikuwa wameenda Uganda kwa kesi moja ya Bw Besigye.
“Ni vigumu kuelewa kwa nini mmoja wa mawakili anaruhusiwa na mwengine kuzuiwa,” akachapisha kwenye mtandao wa X huku akitaka maelezo kutoka kwa serikali ya Uganda.
Bw Lukwago naye alifikishwa mahakamani Jumatano iliyopita akiwa dhaifu siku chache baada ya kukamatwa nyumbani kwake.
Alikana mashtaka ya kushindwa kuripoti kosa la uhaini linalohusiana na kesi ya Bw Besigye, na akaamriwa kusalia rumande gerezani akisubiri kusikilizwa kwa kesi hiyo.
Bw Besigye amekuwa kizuizini akikabiliwa na mashtaka ya uhaini tangu alipotekwa nyara Kenya na kurejeshwa kwa nguvu Uganda mwishoni mwa 2024.
Kutekwa kwake, pamoja na kwa msaidizi wake Obeid Lutale, kulizua mjadala mkali katika eneo la Afrika Mashariki kuhusu mamlaka ya kisheria na masuala ya haki za binadamu.
Bi Karua alikumbana na vikwazo kadhaa kabla ya kuruhusiwa rasmi kumwakilisha Bw Besigye mahakamani. Miongoni mwa changamoto hizo ni ombi lake la awali la kuruhusiwa kufanya kazi ya uwakili nchini Uganda kukataliwa.
“Hapa Kenya, utawala wa Ruto ulimfurush Brian Kagoro, wakili na mwanaharakati. Kule Tanzania walitufurusha pamoja na watu wengi. Hapa Kenya tumewafurusha wengi ukanda wa Afrika Mashariki ikiwemo raia wa Sudan Kusini na hata wa Uturuki,” akasema.
Aidha, mwaka jana alifurushwa Tanzania ili kumzuia kuhudhuria kesi ya kiongozi wa upinzani Tundu Lissu, ambaye pia anakabiliwa na mashtaka ya uhaini.
“Katika haya yote, Kenya imejitokeza kama kitovu cha utekaji nyara na kuwafurusha raia wa kigeni. Kunyimwa kwangu kuingia Uganda naamini ni kinyume cha sheria,” akasema.
Waziri huyo wa zamani alifichua kuwa wakati wa kuzuiliwa kwake, maafisa wa wahamiaji wa Uganda walitaka kumzuilia kwenye seli kabla ya kumhamisha hadi eneo la abiria alikosubiri ndege ya kumrejesha Kenya.
Alidai maafisa wawili wahamiaji walichukua simu yake kwa lazima kabla ya kumrejeshea na maafisa wawili walikaa karibu naye hadi alipoabiri ndege ya kumrejesha Nairobi.
Kabla ya kuabiri ndege, alipewa barua ambayo inampiga marufuku kuingia taifa hilo jirani.
Naibu Rais wa Chama cha Mawakili Uganda Antony Asiimwe ambaye alikuwa amefika kumpokea Bi Karua na wenzake, alishangaa kwa nini alizuiwa kuinga Uganda.
“Hakuna sababu ambazo zilitolewa kumzuia kuingia Uganda. Walimwambia tu hawawezi kumruhusu kuingia Uganda,” akasema Bw Asiimwe.