Dimba

Arsenal waanza kuporomoka

Na MASHIRIKA February 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

ARSENAL imeanza kuandamwa na mikosi inaposaka taji la kwanza la Ligi Kuu Uingereza (EPL) tangu 2004 baada ya kupoteza uongozi wa 2-0 na kulazimishwa sare ya 2-2 na wavuta mkia Wolvehampton mnamo Jumatano usiku.

The Gunners walikuwa wakilenga kufungua mwanya wa alama saba kileleni lakini hilo halikuwezekana, baada ya sare hiyo.

Beki Ricardo Calafiori alijifunga dakika ya nne ya muda wa ziada kipindi cha pili baada ya mnyakaji David Raya na Beki Gabriel kushindwa kuondoa mpira wa juu ndani ya kijisanduku.

Hugo Bueno aliwarejesha Wolves mchezoni baada ya Arsenal kuchukua uongozi kupitia Bukayo Saka na Piero Hincapie.

Saka alisherehekea kandarasi yake mpya ya miaka mitano kupitia bao ambalo alilifunga kwa kichwa kutokana na krosi ya Declan Rice.

Hili lilikuwa bao lake la kwanza akimaliza ukame wa kutofunga katika mechi 15.

Arsenal ilifikiria imemaliza kazi baada ya Hincapie kufunga la pili dakika ya 56 akipokea pasi ya chini kutoka kwa Gabriel.

Saka alitoka kutibiwa na Arsenal ikaanza kulemewa huku Hugo Bueno akichukua nafasi hiyo kufunga bao dakika ya 61.

Wolves waliendelea kuweka presha na Gabriel alimchanganya Raya aliyekuwa akijaribu kuuondoa mpira wa hatari.

Hapo ndipo nguvu mpya Edozie ambaye alikuwa akichezea kikosi cha kwanza cha Wolves kwa mara ya kwanza, aliachilia fataki ambayo ilimgonga Calafiori na ikagonga mlingoti kisha mpira ukajaa ndani ya wavu.

Mechi ikielekea kuisha Arsenal walionekana wakianza kulaumiana wenyewe Gabriel akimsukuma beki mwenzake Yersen Mosquera lakini wakatenganishwa.

Ulikuwa usiku mbaya kwa Mikel Arteta ambaye anasaka taji la EPL kwa mara ya kwanza tangu 2004.

Mashabiki wa Arsenal wameanza kukerwa, wakiandamwa kwa karibu na Manchester City ambayo ina mechi moja ya kuwajibikia huku wakitenganishwa na alama tano pekee.

Arsenal itakabiliana na City kwenye fainali ya Carabao mwezi ujao na pia bado ipo katika Kipute cha Shirikisho la Soka Uingereza (FA) na Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).

Kudondosha alama ni pigo kwa Arsenal ambayo inacheza na Tottenham Hotspur kwenye Debi ya London Jumapili kisha ivaane na Chelsea halafu Brighton.