Habari

Oburu na Sifuna wawania ngome za ODM

Na MOSES NYAMORI June 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAKUNDI hasimu ndani ya Orange Democratic Movement (ODM) yameongeza kasi ya shughuli zao za kisiasa mashinani katika mbio za kuwania udhibiti wa ngome za jadi za chama hicho kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

Kundi linaloongozwa na kiongozi wa ODM, Oburu Oginga, limezindua msururu wa mikutano ya kisiasa ikiwa ni sehemu ya maandalizi ya makubaliano ya muungano na chama cha United Democratic Alliance (UDA) kinachoongozwa na Rais William Ruto.

Kwa upande mwingine, kundi la Linda Mwananchi linaloongozwa na Katibu Mkuu wa ODM limezidisha mikutano yake nchini kote, likijiandaa kwa tangazo kubwa la kisiasa mwezi Septemba ambalo litabainisha kama litaungana na Muungano wa Upinzani unaoongozwa na aliyekuwa Naibu Rais Rigathi Gachagua pamoja na kiongozi wa Wiper, Kalonzo Musyoka.

Katika kikao cha Kamati Kuu ya Uongozi kilichofanyika Jumatatu, kundi la Oburu liliamua kuendeleza kampeni kali ya kusajili wanachama na mikutano ya mashinani ili kuimarisha chama.

Chama kilipanga mkutano wa mashauriano Kwale, ambao unalenga kufufua uungwaji mkono wa ODM katika kaunti hiyo kuelekea 2027.

Taarifa ya chama ilisema lengo ni “ kuimarisha ngome zake kwa maandalizi ya uchaguzi mkuu ujao.”

Mkutano mwingine umepangwa kufanyika Busia Juni 28, ukilenga hasa vijana kutoka maeneo yote saba ya kaunti hiyo kujadili ajenda ya vijana ndani ya ODM.

Wakati huo huo, mrengo wa Sifuna umeandaa mikutano zaidi ya kisiasa kote nchini ambayo itafikia kilele kwa tangazo kubwa Septemba jijini Nairobi.

Mpango huo unalenga kufikia angalau kaunti 24 kabla ya tangazo hilo kuu la kisiasa.

Muungano wa Upinzani, unaoongozwa na Gachagua na Kalonzo Musyoka, tayari umeonyesha nia ya kushirikiana na kundi la Linda Mwananchi katika kuwa na mgombea mmoja wa urais atakayemkabili Rais Ruto.

Kundi hilo limefanya ziara 11 za kisiasa katika maeneo mbalimbali yakiwemo Nairobi, Kitengela, Busia, Kisumu, Mombasa, Machakos na Kakamega.

Wiki iliyopita, viongozi wa kundi hilo akiwemo Sifuna, Gavana James Orengo na Seneta Godfrey Osotsi walifanya mkutano mkubwa Thika, hatua inayoonekana kama kuingia kwao rasmi katika Mlima Kenya.

Osotsi alisema kundi hilo limepanga mikutano zaidi ya 10 kabla ya tangazo la Nairobi mwezi Septemba, akibainisha kuwa wataendelea kusikiliza maoni ya wananchi kabla ya maamuzi ya mwisho ya kisiasa.

Kundi hilo pia limepanga mikutano Meru, Tharaka Nithi, Kilifi, Kwale na hata Eldoret, ngome ya Rais Ruto, kabla ya kufika Siaya, Migori na Homa Bay.

Wanasiasa wapya akiwemo Gavana wa Murang’a Irungu Kang’ata, aliyekuwa Mbunge Alfred Keter na aliyekuwa Katibu Irungu Nyakera wamejiunga na kundi hilo, huku wengine wakitarajiwa kujiunga nalo.

Katika hatua nyingine, Sifuna alisema mazungumzo ya muungano na Upinzani yameshika kasi, huku akisisitiza lengo la kumuondoa Rais Ruto mamlakani katika uchaguzi ujao.

Utafiti wa TIFA uliochapishwa mwezi uliopita ulionyesha kuwa tiketi ya Kalonzo-Sifuna inaungwa mkono wa asilimia 28, ikifuatiwa na Kalonzo-Matiang’i kwa asilimia 31.

Wachambuzi wanasema ushindani ndani ya ODM unaweza kuamua mwelekeo wa kisiasa wa 2027.