Habari

Kindiki awaonya watakaopora na kuharibu mali maandamano ya Juni 25

Na CECIL ODONGO June 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

NAIBU Rais Profesa Kithure Kindiki amesema serikali haitavumulia juhudi zozote za kutumia maandamano ya Gen Z mnamo  Alhamisi kushiriki uporaji na uharibifu wa mali, akionya kuwa watakaofanya hivyo watakabiliwa kisheria.

Profesa Kindiki alisema Katiba inawalinda watakaoshiriki na wale ambao hawatashiriki maandamano kwa hivyo hakuna haja ya kuzua zahama na kutatiza shughuli za wengine.

“Hakuna yeyote atakayetutishia dhidi ya kuwalinda Wakenya ambao wanaendelea na shughuli zao kama kawaida iwe wanasafiri au kuendeleza biashara zao kama kawaida,” akasema Profesa Kindiki.

Makundi mbalimbali yakiwemo wanasiasa wa upinzani wanapanga kuandaa maandamano mnamo Alhamisi kuadhimisha miaka miwili tangu Juni 25, 2024.

Siku hiyo waandamanaji waliokuwa na hasira waliwazidi polisi nguvu na kuingia katika majengo ya Bunge huku wakipinga Mswada wa Fedha 2024 uliokuwa na mapendekezo ya nyongeza ushuru.

Kwa mujibu wa takwimu kutoka Tume ya Kitaifa ya Kutetea Haki za Kibinadamu, Wakenya 60 waliaga dunia kwenye maandamano hayo.

Mnamo Jumapili, Profesa Kindiki alisema Katiba inaruhusu maandamano ila hakutakuwa na nafasi ya mtu yeyote kumvamia mwengine au kuharibu mali na kupora biashara wakati wa maandamano hayo.

“Anayeshiriki na asiyeshiriki wote watalindwa kwa mujibu wa sheria,” akaongeza.

Naibu Rais alikuwa akiongea katika eneobunge la Soy, Kaunti ya Uasin Gishu wakati wa ibada ya madhehebu mbalimbali, hafla ambayo pia ilikuwa ya kuchangishia makanisa 19.

Aliwashutumu baadhi ya wanaoratibu maandamano hayo kwa kueneza uongo kuhusu Mswada wa Fedha 2026 ambao ulipitishwa na wabunge wiki jana.

“Hakuna kifungu kinachopendekeza nyongeza ya ushuru jinsi wanavyodai na hawana msingi wowote wa kudandia kuandamana,” akasema.

Profesa Kindiki pia alirindima ngoma ya ‘Tu Tam’ akiwataka wakazi wa Uasin Gishu kuendelea kumuunga mkono Rais William Ruto ili achaguliwe kwa muhula wa pili mwaka ujao.

“Katiba inasema rais anastahili kuhudumu kwa miaka 10, muhula wa kwanza ni wa kuzindua miradi kisha wa pili ni kukamilisha miradi. Yeyote anayezungumza kuhusu muhula mmoja anakiuka katiba,” akasema.

Kauli hiyo ilirindimwa na viongozi ambao waliandamana naye ambao walisifia serikali kwa kuanzisha miradi mbalimbali maeneo tofauti bila ubaguzi.

Mwenyeji wake, Mbunge wa Soy David Kiplagat alisema Profesa Kindiki ndiye atakuwa mgombeaji mwenza wa Rais Ruto mwakani, akisema juhudi zake kwenye chaguzi ndogo ambazo zimekuwa zikifanyika zilisaidia UDA kutamba.

“Tuna imani na uongozi na utendakazi wa Profesa Kindiki wala hatuna shaka kuwa atachaguliwa mwaka ujao pamoja na Rais ili waendelee kusimamia taifa letu,” akasema Bw Kiplagat.