Wito wakimbizi watambuliwe kama washirika wa maendeleo
HUKU dunia ikiadhimisha Wiki ya Wakimbizi Duniani na Siku ya Wakimbizi Duniani, wito umetolewa kwa jamii na serikali kuwatambua wakimbizi si kama watu wanaohitaji msaada pekee, bali kama washirika muhimu wa maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Refugee-Led Organization Network of Kenya (RELON Kenya), JeanPaul Kasika, amesema wakimbizi wengi nchini wameonyesha ustahimilivu mkubwa kwa kuanzisha biashara, kuunda nafasi za ajira na kuchangia ukuaji wa uchumi katika maeneo wanayoishi.
“Ni wakati wa kubadilisha simulizi kuhusu wakimbizi. Mbali na changamoto wanazopitia, wengi wao ni viongozi, wabunifu, wafanyabiashara na watetezi wa haki za binadamu wanaochangia maendeleo ya jamii,” alisema Kasika.
Kenya imeendelea kuwa makazi ya maelfu ya wakimbizi waliokimbia vita, mateso na ukosefu wa usalama katika nchi zao.
Hata hivyo, wengi wao bado wanakumbana na changamoto za kupata ajira rasmi, elimu, huduma za afya na nyaraka muhimu za kisheria.
Kwa mujibu wa Kasika, dhana kwamba wakimbizi hutegemea misaada pekee imepitwa na wakati.
“Ukweli ni kwamba wakimbizi wengi wanataka kufanya kazi, kujitegemea na kuchangia katika jamii wanazoishi. Kinachowatatiza mara nyingi ni ukosefu wa nyaraka na fursa sawa za kushiriki katika shughuli za kiuchumi,” alieleza.
RELON Kenya, imekuwa ikitetea ushirikishwaji wa wakimbizi katika maamuzi na sera zinazogusa maisha yao.
Kasika alisisitiza kuwa ujumuishaji wa wakimbizi unaweza kuleta manufaa kwa jamii zote mbili za wakimbizi na wenyeji.
“Tunapoadhimisha Wiki ya Wakimbizi Duniani, tuwatambue wakimbizi kama washirika wa maendeleo. Tukikuza mshikamano, usawa wa fursa na ujumuishaji, tutajenga jamii imara zaidi ambapo hakuna anayebaki nyuma,” alisema.
Aliongeza kuwa kutambua mchango wa wakimbizi ni hatua muhimu katika kujenga mustakabali wenye matumaini kwa wote nchini Kenya.