Habari

Ni kivumbi viongozi wa Linda Mwananchi na Linda Ground wakiandaa mikutano tofauti

Na RUSHDIE OUDIA February 21st, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MZOZO uliotikisa chama cha Orange Democratic Movement (ODM) unatarajiwa kuingia hatua mpya leo makundi mawili hasimu yakifanya mikutano tofauti katika maeneo ya Nyanza na Magharibi mwa Kenya.
Kundi moja litakuwa Siaya huku lingine likifanya mikutano Vihiga na Kakamega, hali ambayo imeongeza joto la kisiasa huku madai ya njama za kuvuruga mikutano yakitolewa.
Kiongozi wa chama na Seneta wa Siaya, Dkt Oburu Oginga, ataongoza mkutano wa mrengo wa “Linda Ground” katika mji wa Siaya, umbali wa takriban mita 400 kutoka ofisi ya Gavana James Orengo ambaye anaunga kundi la Linda Mwananchi linaloongozwa na Katibu Mkuu anayepigwa vita Edwin Sifuna.
Hatua hiyo inaonekana kama onyo la moja kwa moja kwa gavana huyo ambaye amekuwa akipinga wazi mpango wa serikali jumuishi na wazo la baadhi ya viongozi wa ODM kushirikiana na Rais William Ruto kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.
Kundi la “Linda Mwananchi” linalojumuisha Bw Orengo, Bw Sifuna na Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino linatarajiwa kufanya mikutano mikubwa katika kaunti za Vihiga na Kakamega.
Kundi hilo linapinga vikali mwelekeo wa chama kuwa na makubaliano ya kabla ya uchaguzi na Rais Ruto, likisisitiza kuwa ODM inapaswa kubaki imara kama chama cha upinzani.
Jana, viongozi wa Linda Mwananchi wakiongozwa na Orengo pamoja na Naibu Kiongozi wa chama Godfrey Osotsi walidai kuwa kuna njama za kuvuruga mkutano wao.
Walisema kuwa lori lao lililokuwa likielekea Kakamega lilivunjwa kioo cha mbele na watu wasiojulikana.
Aidha, walidai kuwa vijana wametumwa kutoka kaunti jirani kuenda Kakamega kwa lengo la kuzua fujo.
Muda mfupi baada ya mkutano wao na wanahabari, kundi la vijana lilijaribu kuvamia hoteli walimokuwa, wakirusha mawe kabla ya polisi kuingilia kati na kuwatawanya kwa kutumia vitoa machozi. Shughuli katika barabara ya Kisumu–Kakamega zilisimama kwa muda mfupi.
Mvutano huo umechochewa zaidi na kauli za viongozi wanaomuunga mkono Rais Ruto, wakiongozwa na Gavana wa Kakamega Fernandes Barasa na Naibu wake Ayub Savula, waliotangaza kuwa hawataruhusu mikutano yoyote itakayovuruga utulivu katika eneo hilo.
Wiki hii, Dkt Oginga aliitisha mkutano wa mashauriano na viongozi kadhaa wa Siaya kama sehemu ya maandalizi ya mkutano wa leo. Hata hivyo, Gavana Orengo hakuhudhuria mkutano huo, ishara ya wazi ya ufa ulio ndani ya chama.
Badala yake, Naibu Gavana William Oduol alihudhuria pamoja na wabunge Gideon Ochanda (Bondo), Elisha Odhiambo (Gem) na Mwakilishi wa Wanawake Christine Ombaka.
Viongozi wengine kutoka vyama tofauti pia walikuwepo, akiwemo Mbunge wa Ugenya David Ochieng na mwenyekiti wa Bodi ya Sukari Kenya Nicholas Gumbo.
Kutohudhuria kwa baadhi ya wabunge mashuhuri kama Otiende Amollo (Rarieda), Samuel Atandi (Alego Usonga), Moses Omondi (Ugunja) na Spika wa Kaunti George Okode kulizua maswali zaidi kuhusu mwelekeo wa chama katika eneo hilo.
Mkutano wa leo unafanyika wiki chache tu baada ya Rais Ruto kukutana na madiwani wa Siaya katika Ikulu ndogo ya Eldoret.
Baada ya mkutano huo, kulienea uvumi kuhusu uwezekano wa hoja ya kumuondoa Gavana Orengo madarakani, madai ambayo yalikanushwa na madiwani waliohudhuria, wakisema Rais alitoa wito wa maelewano na ushirikiano.
Huku wakosoaji wa Orengo wakimlaumu kwa madai ya kusuasua kwa maendeleo katika kaunti, mtangulizi wake, Cornel Rasanga, amemtetea akitaka apewe nafasi ya kutekeleza wajibu wake bila shinikizo za kisiasa.
Leo, macho ya wafuasi wa ODM na wachambuzi wa siasa yataelekezwa Siaya, Vihiga na Kakamega kuona ni kundi lipi litakaloonyesha nguvu zaidi. Mgawanyiko huo umeiweka ODM katika njia panda, huku hatma ya chama na mwelekeo wake kuelekea 2027 ukiwa kitendawili kinachosubiri majibu.