HabariHabari za Kitaifa

Ruto awataka viongozi kuzika tofauti zao

Na KEVIN CHERUIYOT February 22nd, 2026 Kusoma ni dakika: 1

RAIS William Ruto Jumapili, Februari 22, aliwataka viongozi wa chama cha UDA katika Kaunti ya Kiambu kuupa umuhimu utoaji wa huduma badala ya uhasama kisiasa.

Akizungumza katika maadhimisho ya tatu ya kanisa la Jesus Compassion Ministries (JCM) mjini Ruiru, Rais alirai viongozi wa Kiambu kuweka kando tofauti zao za kisiasa na kuzingatia kuhudumia mamilioni ya Wakenya waliowaaminia kura zao.

“Nataka viongozi wote wanisikize –kutoka kwa madiwani hadi magavana, mbunge, seneta, mwakilishi wa kike na mimi binafsi kama rais. Sisi ni wafanyakazi wa watu wa Kiambu na Wakenya wote. Kama kazi haitafanywa, ni sisi wa kulaumiwa,” alisema Rais Ruto.

Gavana wa Kiambu Kimani Wamatangi na Mbunge wa Thika Town, Alice Ng’ang’a ambao wametofautiana vikali hapo mbeleni walikuwepo vilevile.

“Usitafute mtu wa kulaumu. Ikiwa kuna kazi ya kufanya Kiambu, ni sharti tufanye kazi pamoja. Sitakubali kazi ihujumiwe ilhali tuna viongozi wenye uwezo,” alisema.

“Kama kuna suala Githurai, tusilaumiane. Tutatue tatizo hilo kama timu. Mna wajibu wa kusuluhisha matatizo ya Kaunti ya Kiambu,” alisema.

Rais vilevile aliwahakikishia wakazi kwamba mikakati imepangwa kuhakikisha manifesto ya serikali ya Kenya Kwanza inatekelezwa.

Kiambu, sawa na sehemu nyingine nchini. Akiadhimisha miaka mitatu tangu kanisa hilo lilipoanzishwa, Rais alitoa mchango wa Sh9 milioni utakaosambazwa katika awamu za Sh3 milioni kila mwaka na kuahidi Sh5 milioni za ziada kwa mpango wa NYOTA wa kanisa hilo.