Habari

Ilikuwa mikate hewa? Jinsi kampuni ya uokaji ilivyokula kavu kesi iliyoshtaki shule ya Kaimosi

Na RUSHDIE OUDIA February 24th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

KILICHOANZA kama kesi ya kudai malipo ya Sh845,378 kwa mkate na unga wa ngano kiligeuka funzo ghali kuhusu umuhimu wa stakabadhi zinazohitajika kisheria, kampuni moja ya uokaji mikate ikikagharimika pakubwa.

Kampuni kwa jina Alicia Bakers and Confectioners iliwasilisha kesi kortini kudai shule ya Friends School Kaimosi Sh845, 378 kwa bidhaa za mkate na unga wa ngano ilizodai kuwasilisha shuleni humo kati ya Januari 1, 2016 na Mei 25, 2023.

Agosti 8, 2025, korti ya hakimu ilitoa hukumu iliyoegemea mwokaji na kuamuru Friends School Kaimosi kulipa Sh845,378 na gharama ya ziada ya Sh40,000.

Shule ilikata rufaa katika Mahakama ya Madeni ya kiwango cha chini, Siaya, mnamo Septemba 3, 2025, kwenye kesi iliyofichua mianya kwenye michakato ya ununuzi na kuathiri uadilifu wake.

Bodi ilihoji kuwa hakimu alikosea katika hukumu yake iliyompendelea mwokaji pasipo ushahidi thabiti kuonyesha bidhaa ziliwasilishwa.

Aidha, shule ilisema kuwa kandarasi kati yake na kampuni ya uokaji ilisheheni makosa tele, ukiukaji taratibu na kanuni kisheria, ikihoji kuwa, kutekeleza malipo hayo kutakuwa sawa na kuhalalisha na kusafisha mchakato wenye walakini kisheria.

Mhasibu wa Alicia bakers, Kevin Amollo, aliwasilisha kortini barua za kudai malipo, nakala za kuitisha malipo na kuitisha bidhaa (LPO) zilizotumwa Juni 24, 2018, nakala za benki na hundi.

Miongoni mwa stakabadhi hizo, ilikuwepo nakala ya kuwasilisha mifuko 100 ya kilogramu 50 ya unga wa ngano, ambayo haikuwa na LPO thabiti kwa sababu LPO ya awali muda wake ulikamilika Juni 24, 2016.

Bw Amollo vilevile alikiri kampuni haikumiliki vyeti vya kuthibitisha uwasilishaji wa bidhaa. Alitoa ushahidi kuwa nakala za bidhaa ziliwekwa muhuri na saini na mkutubi aliyehudumu kwa kandarasi kati ya 2016 na 2019.

Katika hukumu iliyotolewa Februari 5, 2026, jaji David Kemei alisisitiza kwamba korti za kisheria zinaongozwa na ushahidi – siyo huruma wala kukisia. Alihoji kuwa nakala na LPOs zilizowasilishwa hazitoshi, kivyake, kuthibitisha kwamba shule ilipokea bidhaa.

Mwishowe, korti iliruhusu rufaa ya shule, ikafuta uamuzi wa hakimu na kutupilia mbali madai ya mwokaji.

“Mkata rufaa hawezi kukosolewa kwa kusisitiza kuhusu ushahidi huo kutoka kwa mlalamishi. Shirika hilo hivyo basi halipaswi kuruhusiwa kunufaika kutokana na biashara ambayo haikuthibitishwa na nakala zinazohitajika,” alisema jaji.