Kocha Belinda ataja kikosi cha Harambee Starlets akilenga Kombe la Dunia 2027
KOCHA wa Harambee Starlets, Beldine Odemba Alhamisi, alitaja kikosi cha muda cha wachezaji 29 kitakachoanza maandalizi ya fainali za Kombe la Mataifa ya Afrika kwa Wanawake (WAFCON) zitakazofanyika Morocco kuanzia Julai 26 hadi Agosti 16.
Wachezaji hao wanatarajiwa kuripoti kambini Jumatatu hii huku Kenya ikijiandaa kushiriki mashindano hayo kwa mara ya pili baada ya kucheza kwa mara ya kwanza 2016 nchini Cameroon.
Odemba amedumisha kikosi kilichoshiriki mechi za awali dhidi ya Zambia na Lesotho mapema mwezi huu, huku akiwajumuisha tena mastaa wa Trinity Starlets, Lilian Adhiambo na Elizabeth Muteshi.
Pia amewaamini chipukizi waliopitia vikosi vya chipukizi na sasa wanazidi kujizolea nafasi katika timu ya taifa. Miongoni mwao ni Fasila Adhiambo, Marion Serenge, Elizabeth Mideva, Elizabeth Muteshi na Elizabeth Ochaka.
Starlets watafungua kampeni yao dhidi ya wenyeji Morocco Julai 26 katika Uwanja wa Moulay El Hassan mjini Rabat kuanzia saa tano usiku saa za Kenya.
Baadaye watachuana na Senegal Julai 30 katika Uwanja wa Olympic kuanzia saa mbili usiku kabla ya kukamilisha mechi za Kundi A dhidi ya Algeria Agosti 3 katika uwanja huo huo kuanzia saa tano usiku.
Odemba amesema timu inalenga kufika angalau nusu fainali, hatua ambayo itaipa Kenya nafasi ya kushiriki Kombe la Dunia la Wanawake la FIFA kwa mara ya kwanza mwakani nchini Brazil.
“Kuwakilisha Kenya katika WAFCON ni heshima kubwa. Tunalenga kufika nusu fainali kwa sababu hatua hiyo itatufungulia mlango wa kushiriki. Hilo ndilo tutapigania,” alisema Odemba.
Aliongeza kuwa Starlets itapambana kwa nguvu, kuendelea kuboresha kiwango chake na kuhakikisha inaipeperusha vyema bendera ya Kenya katika mashindano hayo ya bara.
Kikosi cha muda
Walinda lango
Annedy Kundu, Lilian Awuor, Vivian Shiyonzo, Lilian Adhiambo
Mabeki
Leah Andiema, Elizabeth Ochaka, Ruth Ingosi, Vivian Nasaka, Enez Mango, Euphrasier Shilwatso, Norah Ann, Elizabeth Muteshi, Mary Nthambi
Viungo wa Kati
Mwanalima Adam, Martha Amunyolete, Tereza Engesha, Fasila Adhiambo, Shaline Nambengele, Lorna Nyarinda, Mercy Airo, Airin Madalina
Washambuliaji
Shirleen Opisa, Eglay Mukhwana, Elizabeth Mideva, Marion Serenge, Violet Nanjala, Valerie Nekesa, Catherine Khaemba, Tumaini Waliaula