Maoni

MAONI: Viongozi wachanga wana kiu kubwa ya kuchukua uongozi 2027

Na HELLEN NJAGI February 25th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MRENGO wa kisiasa wa ‘Linda Mwananchi’ umezua msisimko mkubwa wa kisiasa katika siasa za humu nchini.Siasa za mrengo huu zimeashiria kuleta mwanga wa ukombozi na kuondoa dhana ya kuwa vijana ni viongozi wa kesho tu.

Iwapo chama cha ODM kitawaondoa wanachama wake wanaoonekana kuwa waasi, hicho kitakuwa kichocheo cha kuimarisha umaarufu wao na huenda wakapata wafuasi wengi zaidi hasa wapigakura wa kizazi kipya.

Kuondolewa kwao kutatonesha jeraha kubwa si kwa ODM pekee bali kwa chama cha UDA ambacho kinatarajia ndoa yake na ODM ikipe nguvu za kuupiku upinzani.

Kuna uwezekano mkubwa mrengo huo wa Linda Mwanachi umejengwa kisiri begani mwa wanasiasa wakongwe katika nchi hii.

Wanazo hela za kuandaa mikutano na kufanya misafara mikubwa katika maeneo tofauti nchini.

Fedha hizi zanatoka wapi? Huenda mpinzani mkuu wa UDA katika uchaguzi wa 2027 atakuwa mwanasiasa chipukizi wala si wale wakongwe ambao Wakenya wengi wamewazoea.

Mrengo wa Linda Mwananchi ni uvuvio wa mageuzi unaolenga kuleta damu changa katika siasa za Kenya.

Hili limedhihirika katika uungwaji mkono wa wanasiasa chipukizi katika mrengo huo ambao kwa muda mfupi wameweza kufanya mikutano yenye halaiki ya watu katika maeneo ya Busia, Kitengela na Kakamega.

Kundi hili huenda likakosa kupewa uzito wa kisiasa kwa sasa lakini si la kupuuzwa. Limeshika kasi upesi hasa kwa kukivutia kizazi cha Gen-Z na Wakenya wenye hamaki za kudhulumiwa na hali ngumu ya kiuchumi.

Vigogo wa vyama vya upinzani wana mchango katika kuimarika kwa mrengo huu wa Linda Mwananchi. Wamekwisha kutathmini uwezo wa kila mmoja wao.

Ni bayana kuwa Bw Kalonzo Musyoka hajatifua kivumbi kuonyesha ari ya uwaniaji. Kapu la kura la Dkt Fred Matiang’i halina hakikisho.

Ushawishi wa Eugene Wamalwa katika eneo la Magharibi hauna mashiko nayo nyota ya Bw Rigathi Gachagua ingali imesakamwa na kubanduliwa kwake enzini.

Vigogo wa upinzani watajivunia kadi hii ya wanasiasa wachanga mradi tu upinzani upate ushindi.

Endapo umaarufu wa Linda Mwananchi utaendelea hadi mwaka wa 2027, upinzani hautakuwa na jingine ila kukusanya kura za ngome zake na hatimaye kumteua mgombea urais mchanga atakayempa Rais William Ruto upinzani wa kustaajabisha.

Rais Ruto naye si mchache, ana uelewa mkubwa wa sataranji ya siasa. Ashafanya jaribio katika ngome ya Mlima Kenya kunakoonekana kuibuka upinzani na kufahamu mbinu atakazotumia kunasa kura za eneo hilo.

Hata hivyo, chama cha UDA kitakabiliwa na upinzani mkali ifikapo 2027.

Mwamko wa kizazi kichanga kinachotaka mabadiliko, wapigakura wapya wasiotambua siasa kongwe za nchi wala kuwa na subira ya kungoja ahadi batili za wanasiasa ni kizingiti kikubwa kwa chama cha UDA kupata ushindi.

Kupiga kura kwa kizazi kipya kutapunguza idadi ya wabunge waliopo bungeni sasa na kuleta sura mpya katika bunge.

Kufikia sasa, kadi zenye thamani kubwa kumpa Rais Ruto ushindani mkali ni za Edwin Sifuna, Babu Owino, Natembeya, Mohamed Ali, vigogo wa siasa Richard Onyonka, James Orengo na wengine katika mrengo wa Linda Mwananchi.

Wimbi la mageuzi linabisha na viongozi wachanga wameonyesha ari kubwa kuiondoa sura kongwe ya siasa za humu nchini