Matiang’i ajeruhi ODM nyota yake iking’aa nyumbani
MGOMBEA urais wa chama cha Jubilee, Fred Matiang’i, amefurahia mafanikio ya ziara yake ya siku tatu katika eneo la Gusii, ambapo aliandamana na viongozi wa Muungano wa Upinzani.
Dkt Matiang’i alitumia ziara hiyo kuonyesha ubabe wake kama kigogo wa siasa za eneo hilo ambalo lilichukuliwa kuwa ngome ya chama cha ODM.
Dkt Matiang’i pia aliapishwa kuwa msemaji wa jamii ya Abagusii na Baraza la Wazee wa Abagusii. Wataalamu wa siasa wanasema kuwa hii ni hatua kubwa kwake kwani inaendana na desturi za Abagusii zinazohusu mamlaka na uongozi.
Wataalamu wanasema kuwa, kufuatia ziara hii, Dkt Matiang’i amegeuka kuwa kiongozi makini anayejua kusoma hadhira na kutoa ujumbe wazi wa kisiasa katika eneo ambalo chama cha ODM kinawakilishwa na viongozi wawili wakuu, Gavana Simba Arati ambaye ni naibu kiongozi na Timothy Bosire ambaye ni mweka hazina wa kitaifa wa chama hicho cha chungwa.
Mikutano iliyojaa msisimko mkubwa ilivutia umati mkubwa wa watu, ikiongozwa na seneta wa Kisii, Richard Onyonka na mwenzake wa Nyamira, Okong’o Omogeni.
Wabunge Clive Gisairo (Kitutu Masaba), Patrick Osero (Borabu), Anthony Kibagendi (Kitutu Chache South), Innocent Obiri (Bobasi), Obadiah Barongo (Bomachoge Borabu) na Dkt Charles Onchoke (Bonchari) walimfuata Dkt Matiang’i huku viongozi wengine wa vyama mbalimbali wakijiunga naye.
Wagombea kadhaa, wakiwemo waliokuwa wapinzani wake wakali, wakiongozwa na aliyekuwa Waziri wa Elimu ambaye sasa anawania ugavana Kisii, Ezekiel Machogu, pia walijiunga na msafara huo.
Wagombea wengi wameamua kumsaidia Dkt Matiang’i katika kinyang’anyiro cha urais kwa matarajio ya kushinda viti.
Mikutano hiyo imerudisha kumbukumbu za Simeon Nyachae, kiongozi wa zamani wa chama cha Ford People na mbabe wa kisiasa eneo la Gusii, aliyegombea urais mnamo 2002 na kuibuka katika nafasi ya tatu baada ya Mwai Kibaki na Uhuru Kenyatta.
Nyachae alirai jamii nzima kumuunga mkono, akihakikisha Wabunge wote 10 walichaguliwa kwa tiketi ya chama chake.
Wachanganuzi wanasema mikutano iliyofanyika katika Nyamira na Kisii inatoa ujumbe wa kisiasa kwamba wanasiasa wasioungana na Dkt Matiang’i wanaweza kukumbana na changamoto za kisiasa katika uchaguzi wa 2027.
“Mwanzo, Dkt Matiang’i amekuwa kiongozi mkuu wa Abagusii muda mrefu baada ya Nyachae. Ziara yake pia imeleta nguvu kwa chama cha Jubilee katika eneo la Gusii. Yeyote anayetamani kushinda kiti cha uchaguzi Gusii 2027 lazima aungane na Matiang’i na chama cha Jubilee,” alisema mtaalamu wa siasa Omondi Okumu.
Mtaalamu mwingine, Dismas Mokua, alisema Dkt Matiang’i ni mgombea urais wa Jubilee 2027 kisheria na anapanga kuwa mgombea urais wa Muungano wa Upinzani.
Ziara ya Kisii/Nyamira ni sehemu ya mkakati wa kitaifa kuhakikisha anapata uungwaji mkono wa jamii ya Abagusii kabla ya kampeni za kitaifa.
Gavana wa Kisii, Simba Arati, ambaye pia ni naibu kiongozi wa ODM, Mbunge wa South Mugirango Silvanus Osoro, Japheth Nyakundi na Mbunge wa Nyaribari Chache Zaheer Jhanda wa UDA wanatarajiwa kupambana na wimbi la Dkt Matiang’i.
Miongoni mwa maeneo ambayo msafara wa Dkt Matiang’i ulitembelea ni Nyamache, nyumbani kwa Gavana Arati.
Huko, wakazi wa Bobasi walijitokeza kwa wingi kumpokea Dkt Matiang’i na kushutumu Gavana Arati kwa uongozi duni.
Viongozi wa upinzani walimshutumu Arati kwa kuwazuia kutumia uwanja wa Gusii.
Wataalamu wanasema changamoto kubwa kwa Dkt Matiang’i ni kuunda mtandao wa kitaifa ili kuonyesha uwezo wake wa kushindana kisiasa na Rais Ruto.