Habari za Kitaifa

Mamluki Mkenya adai Warusi wanamtafuta wakitaka kumuua

Na SIMON CIURI February 27th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

FESTUS Omwamba, mwanamume anayeshukiwa kuhusika na ulanguzi wa binadamu, amedai kuwa alijisalimisha kwa polisi wa Kenya mjini Moyale baada ya kupokea vitisho vya kuuawa kutoka kwa watu wasiojulikana ila ni raia wa Urusi.

Jana, mahakama ya Kahawa iliagiza mawakili wanaomwakilisha Omwamba anayemiliki kampuni ya Global Face Human Resources, warudi mahakamani leo ili kuuliza maswali maafisa wa uchunguzi kuhusu vitisho alivyoibua.

Kiongozi wa mashtaka aliomba mahakama isimwachilie Omwamba kwa dhamana ili aweze kulindwa huku uchunguzi kuhusu ulanguzi wa binadamu ukiendelea, ambapo Omwamba, 33, ni mshukiwa mkuu.

Polisi na maafisa wa ujasusi wanaamini kuwa Omwamba ndiye kiongozi wa mtandao wa kimataifa wa usafirishaji haramu wa binadamu ambao umefanya angalau Wakenya 1,000 kujiunga na jeshi la Urusi ili kupigana Ukraine.

Mahakamani, Omwamba alikataa kuhusika katika usafirishaji haramu wa binadamu.

Kikosi cha mawakili wake kilipinga kukamatwa kwake, wakieleza kuwa tayari ana dhamana ya Sh100,000 iliyotolewa na Mahakama Kuu mnamo Februari 4.

Mahakama Kuu ya Nairobi pia ilizuia kukamatwa kwake.

Alipofika mahakamani jana, Omwamba alionekana mwenye furaha huku akisalimiana na waandishi wa habari nje na ndani ya mahakama, licha ya kukabiliwa na kesi ya ulanguzi wa binadamu ambayo adhabu yake ni kifungo cha miaka 30 jela au faini ya Sh30 milioni akipatikana na hatia.

Upande wa mashtaka kupitia hati ya kiapo ya Konstebo wa polisi Robi Stella, iliambia mahakama kuwa wanapinga Omwamba kuachiliwa kwa dhamana, wakisisitiza kuwa anaweza kuingilia ushahidi.

“Uchunguzi bado unaendelea, na mshitakiwa anaweza kuingilia mchakato ikiwa ataachiliwa. Waathiriwa waliookolewa wanaweza kutishwa, kujeruhiwa, au kushurutishwa kutojitokeza ikiwa mshukiwa ataachiliwa,” DCI ilisema.

Kiongozi wa mashtaka pia alisema kumzuilia rumande kunaweza kuwa njia bora ya kumlinda Omwamba dhidi ya vitisho vya kifo kutoka kwa raia wa Urusi alivyodai.

“Mshukiwa alidai alipokea vitisho vya kifo. Kwa usalama wake, anapaswa kuwekwa ndani. Alifika kwa afisa wa uchunguzi akieleza hofu baada ya kupokea vitisho kutoka kwa raia wa Urusi. Kuzuiliwa rumande ni kwa ulinzi wake. Makazi yake hayajathibitishwa,” kiongozi wa mashtaka aliambia mahakama.

Lakini mawakili wa Omwamba walipinga hoja hiyo, wakisema Omwamba alijisalimisha kwa hiari wala hakuwa katika hatari ya kutoroka.

Waliongeza kuwa mshukiwa yu tayari kuweka pasipoti yake kortini.

Hakimu aliamua kuwa amri ya Mahakama Kuu iliyotolewa awali ilizuia mshukiwa kukamatwa uchunguzi ukiendelea, na haikumzuia kusomewa na kujibu mashtaka.

Ripoti ya Huduma ya Kitaifa ya Ujasusi iliyowasilishwa kwa wabunge mnamo Februari 18, 2026, ilionyesha kulikuwa na amri ya kumzuia Omwamba kusafiri kwa jukumu lake la kupeleka Wakenya kuajiriwa na Urusi kupigana Ukraine.

Haijabainika Omwamba alivyoweza kusafiri mara kwa mara kwenda Urusi licha ya kuwepo kwa amri hiyo.

Mikhail Lyapin, raia wa Urusi anayechukuliwa na maafisa kuwa ni mshirika wa kibiashara wa Omwamba, alikamatwa Septemba 24, 2025 baada ya msako katika nyumba moja mtaani Greatwall Apartments, Athi River.

Wakati wa operesheni, polisi walikuta Wakenya 22 katika nyumba hiyo, ambao walikuwa wametayarishwa kusafiri Moscow kujiunga na jeshi la Urusi.

Edward Gituku, anayechukuliwa kuwa mshirika wa Omwamba, pia alikamatwa.

Mnamo Jumanne, Omwamba aliambia Taifa Leo alikuwa Urusi, ambapo amekuwa akifanya kazi kwa miezi kadhaa kama msimamizi katika kampuni ya usafi na angerudi Kenya Machi kwa kesi aliyowasilisha mwaka jana kuzuia kukamatwa.