Uchunguzi waanza kuhusu ndege iliyomuua mbunge
MAAFISA wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (KCCA) na Mkurugenzi wa Idara ya Upelelezi Nchini (DCI) Jumapili Machi 1, 2026 walianza uchunguzi katika eneo ambako Mbunge wa Emurua Dikirr Johana Ngéno na watu wengine watano waliaga dunia kupitia ajali ya helikopta.
Mabaki ya ndege hiyo ambayo iliteketea, yalizingirwa huku vikosi kutoka KCCA na DCI vikiondoa vifaa muhimu vya kiufundi ambavyo vitasaidia kubaini kilichosababisha ajali hiyo.
Kamanda wa Polisi wa Kaunti ya Nandi Samuel Mukuusi na Idara ya Kufuatilia Ajali za ndege, zilipata mashine ya GPS, vifaa vya kuabiri ndege na vifaa vingine muhimu ambavyo vitachunguzwa kitaalamu.
Wachunguzi wanalenga kujua iwapo ni tatizo la kiufundi, hali mbaya ya hewa au rubani ndiye alisababisha ajali hiyo.
“Eneo la tukio limezingirwa ili uchunguzi wa ndani ufanyike,” akasema Bw Mukuusi.
Kutokana na kuteketea sana, ni chuma zilizotapakaa ndizo zilipatikana kwenye msitu wa Nandi Kaskazini eneo la Chepkiep eneobunge la Mosop, Kaunti ya Nandi.
Pia wachunguzi wamerekodi taarifa kutoka kwa wanakijiji ambao walishuhudia ndege hiyo ikianguka, na pia wanatathmini jinsi ambavyo ilikuwa ikitawala anga.
Jana, Machi 1, 2026, wamiliki wa ndege hiyo walifika katika eneo la ajali na kushirikiana na vyombo vya usalama kuendesha uchunguzi.
Huzuni ilitanda katika Hospitali ya Mafunzo na Rufaa ya Eldoret wakati ambapo miili ya Bw Ng’eno na watu wengine watano ilikuwa ikihamishwa hadi makafani ya Lee Nairobi.
Wahudumu wa mochari waliweka mabaki ya walioangamia katika majeneza sita huku familia, maafisa wa serikali, polisi, wanasiasa na wafuasi wakitazama kwa uchungu.
Kati ya waliokwepo ni magavana Jonathan Bii (Uasin Gishu), Stephen Sang’ (Nandi), Patrick Ole Ntutu (Narok), Naibu Gavana wa Narok Tamalinye Koech, Kamanda wa Kaunti Benjamin Mwanthi na wabunge wengi kutoka kaskazini na kusini mwa Bonde la Ufa.
Saa nane mchana, gari lililobeba majeneza hao sita liliondoka MTRH likiwa limesindikizwa na wanasiasa, maafisa wa serikali, polisi na kundi kubwa la waombolezaji.