Wakazi wataka kulipwa fidia kabla ya ujenzi wa Daraja la Nithi
WAKAZI 28 watalazimika kuikabidhi serikali ardhi yao ndani ya wiki mbili zijazo ili kufungua nafasi kwa ujenzi wa Daraja la Nithi katika Kaunti ya Tharaka Nithi.
Baada ya hapo watasubiri kulipwa fidia kwa sababu Tume ya Kitaifa ya Ardhi (NLC) tayari imewapa notisi ya kuondoka kwenye ardhi hizo.
Hatua hiyo imechukuliwa licha ya Rais William Ruto hivi majuzi kuwahakikishia wananchi kuwa serikali ilikuwa imekamilisha mchakato wa kuwalipa fidia wamiliki wa ardhi walioathiriwa na mradi huo.
“Tumetenga Sh7 milioni kwa ajili ya ujenzi wa Daraja la Nithi na mwanakandarasi tayari yuko eneo la mradi. Pia tumekamilisha mchakato wa kutoa fidia na kazi ya kujenga daraja hilo inaendelea ili kumaliza tatizo ambalo limesabaisha maisha ya watu yapotee kwa zaidi ya miaka 30,” akasema Rais Ruto akiwa Kaunti ya Meru Jumapili.
Imebainika kuwa Tume ya Kitaifa ya Ardhi Nchini (NLC) imetumia Kifungu cha 120(2) cha Sheria ya Ardhi kinachoiruhusu serikali kuchukua umiliki wa ardhi ya binafsi kabla ya kulipa fidia.
Hatua hiyo ina maana kuwa serikali imeutangaza mradi wa Daraja la Nithi kuwa wa dharura, ambao kucheleweshwa kwake kungekuwa kinyume na maslahi ya umma.
Mkazi Munene Njeru, amesema kuwa walitarajia walipwe pesa baada ya rais kusema mchakato wa kutoa fidia ulikuwa umekamilika.
“Mbona serikali ina pesa kuwalipa wanakandarasi ilhali hakuna bajeti kwa wamiliki wa ardhi? Tumeingiwa na wasiwasi kwa sababu rais amesema fidia imeshatolewa,” akasema Bw Njeru.