Dimba

Siri ya Carrick ugani Old Trafford iliyorejesha makali ya Man United EPL

Na MASHIRIKA March 3rd, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MICHAEL Carrick anazidi kupokea mavuno ya matokeo bora kutoka kwa wachezaji wake wa Manchester United kufuatia uamuzi ambao wakufunzi wa awali wa kikosi hicho, wakiwemo Louis van Gaal na Erik ten Hag, walichelea kufanya.

Kiungo huyo wa zamani wa Man-United ameibua msisimko na kuchangia pakubwa ufufuo wa makali ya miamba hao tangu achukue mikoba ya ukocha kutoka kwa Ruben Amorim hadi mwishoni mwa msimu huu.

Carrick, 44, alirejea Old Trafford katikati ya Januari mwaka huu na ameongoza vijana wake kushinda mechi sita kati ya saba zilizopita katika Ligi Kuu ya Uingereza (EPL).

Alama 19 kati ya 21 ambazo Man-United wamejizolea katika michuano hiyo zimewapandisha jedwalini hadi nafasi ya tatu na sasa wanajivunia pointi 51, sawa na nambari nne Aston Villa ambao pia wametendaza jumla ya mechi 28.

Ilivyo, Man-United kwa sasa wana nafasi nzuri zaidi ya kufuzu kwa kipute cha Klabu Bingwa Ulaya (UEFA) muhula ujao licha ya presha kali kutoka kwa Villa, Liverpool, Chelsea na Brentford.

Tangu arejee Man-United, Carrick amefanya mabadiliko mengi makubwa yanayozidi kuwapa mashabiki matumaini na kitu kipya zaidi cha kufuatilia katika kikosi chao.

Pamoja na kusalia kuwa miongoni mwa klabu zinazowania fursa ya kukamilisha kampeni za EPL msimu huu ndani ya mduara wa nne-bora, matokeo bora ya Man-United ni ithibati tosha kuwa kikosi hicho kinazidi kuwa thabiti na imara.

Baada ya kupokeza Manchester City kichapo cha 2-0 ugani Old Trafford mnamo Januari 17, Man-United walikomoa Arsenal (3-2), Fulham (3-2) na Tottenham Hotspur (2-0) kwa usanjari huo.

Ingawa West Ham United waliwalazimishia sare ya 1-1 uwanjani London Stadium mnamo Februari 10, vijana wa Carrick walijinyanyua upesi na kucharaza Everton 1-0 kabla ya kunyuka Crystal Palace 2-1 wikendi jana.

Anapowajibisha kikosi chake uwanjani, Carrick ametupilia mbali mfumo wa 3-4-3 uliokumbatiwa sana na Amorim huku akimrejesha sasa kiungo chipukizi Kobbie Mainoo, 20, kwenye kikosi cha kwanza.

Nje ya uwanja, kocha huyo amechukua uamuzi wa kuhutubia wachezaji wake kila baada ya mechi, jambo ambalo Amorim hakuwa na mazoea ya kufanya.

Ingawa amekuwa akitenga muda kwa ajili ya uchambuzi wa kina wa matokeo ya kila mchuano katika siku inayofuata, Carrick ameteua kimakusudi kuelekeza juhudi zake kuimarisha uthabiti wa kiakili wa wanasoka wake.

Akiwa nao katika chumba cha kubadilishia nguo, kila mchezaji huwa huru kutoa maoni yake huku wenyewe wakikosoana kwa heshima na mahitaji ya kila mmoja yakishughulikiwa kwa msingi wa utu.

Zaidi ya hayo, Carrick amefutilia mbali mfumo uliokumbatiwa na Ten Hag na Amorim wa kulazimisha wachezaji wa Man-United kushiriki vipindi viwili vya mazoezi siku moja baada ya mechi.

Badala yake, mkufunzi huyo ameanzisha mfumo wa kutenga siku maalumu za mapumziko ndani ya saa 24 baada ya kukamilika kwa mchuano.

Isitoshe, vipindi vya kurejesha hali za mwili na uponyaji wa misuli miongoni mwa wachezaji sasa vimeratibiwa kufanyika ndani ya siku mbili mwishoni mwa kila pambano.

Kwa mujibu wa gazeti la The Telegraph, uamuzi huo umepokelewa vyema na kikosi kizima huku wachezaji wakihisi kwamba sasa wanaweza kufurahia kila ushindi wanaousajili kwa kupiga sherehe ya saa chache kabla ya kurejea kazini wakiwa na ari, nguvu na umakini zaidi.

Inaripotiwa kuwa ukosefu wa huruma na utu kutoka kwa wakufunzi wa zamani wa Man-United, kuanzia kwa Van Gaal hadi kwa Ten Hag ni jambo jingine lililoathiri wachezaji wa Man-United kisaikolojia kwa kipindi kirefu.

Lakini inadaiwa kwamba Carrick anaelewa kwamba kila mchezaji anahitaji kuonyeshwa upendo na heshima ndipo naye apende na kuheshimu wenzake pamoja na wote wanaomsimamia.

Chanzo kimoja kilisema: “Wachezaji wanaingiliana vizuri sana. Kila mmoja anajali maisha ya mwenzake. Hata wanapokabiliwa na changamoto, wapo radhi kumzungumzia kocha ambaye yuko tayari kuwasilikiliza na kuwaelekeza ipasavyo kwa sababu ana maslahi yao moyoni.”

Man-United wameratibiwa kuchuana na Newcastle United, Villa na Bournemouth mwezi huu kabla ya kufungua kampeni zao za Aprili dhidi ya Leeds United ugani Old Trafford.

Akizungumza na wanahabari mwishoni mwa mechi iliyowakutanisha na Palace mnamo Jumapili, Carrick alisema: “Nadhani tuko mahali pazuri jedwalini. Kwa namna fulani, tumepiga hatua kubwa na kushinda mechi ambazo huenda kikosi kingepoteza nyakati fulani hapo nyuma. Natumai tutaendelea kucheza vyema na kujiimarisha zaidi hatua kwa hatua. Tuendelee kutarajia mambo mazuri.”