Liverpool hohehahe mbele ya mbweha, Everton, Sunderland wakiwika EPL
RODRIGO Gomes na Andre walifunga mabao mawili dakika za jioni na kusaidia wavutamkia Wolvehampton Wanderers kungária Liverpool 2-1 uwanja wa Molineux katika mechi ya Ligi Kuu Uingereza (EPL) Jumanne usiku.
Kichapo hicho kiliwaacha Liverpool kwa alama 48 kutokana na mechi 29 wakiwa nambari tano katika msimamo wa jedwali.
Kuimarika kwa Wolves kumewafikisha alama 16 katika mechi 30 japo bado wapo mkiani mwa EPL. Kupigwa na Wolves kulikuwa kichapo cha tisa kwa vijana wa Arne Slot msimu huu.
Kwa muda wa miaka 10 Liverpool hawajapoteza mechi 10 kwa msimu.
Iwapo Chelsea na Aston Villa zitashinda Jumatano usiku, basi Liverpool watashuka hadi nafasi ya sita na kuwa nje ya timu zinazolenga kufuzu Klabu Bingwa Ulaya (UEFA).
Hakuna shaka kuwa Wolves wameimarika chini ya Kocha Rob Edwards na mabao yao yalizima lile lililofungwa na Mohamed Salah ambaye alimaliza ukame wa kutofunga katika mechi 10.
Liverpool na Wolves zitakutana tena Ijumaa katika raundi ya tano ya FA ugani Molineux.
“Ni matokeo mabaya kwa sababu katika kipindi cha kwanza tulitawala sana mchezo huu. Tulibuni nafasi nyingi za kufunga lakini hatukuwa na bahati,” akasema Slot.
“Tunapoteza mechi nyingi na kudondosha alama lakini sasa Ijumaa lazima tulipize kisasi,” akaongeza Slot.
Katika mechi nyingine, Everton ilitamatisha rekodi mbaya ya kutoshinda katika mechi saba na kushinda Burnley 2-0.
Ushindi kwenye mechi hiyo iliyogaragazwa katika uwanja wao mpya wa Hill Dickinson uliimarisha nafasi yao ya kufuzu kwa soka ya Bara Ulaya.
Mabao ya James Tarkowsky kupitia kichwa kipindi cha kwanza na Kieran Dewsbury Hall kipindi cha pili yaliwapa Everton ushindi wao wa kwanza wa nyumbani baada ya miezi mitatu na sasa wapo alama mbili nyuma ya Chelsea.
Leeds United nao watakaza meno zaidi kunusurika shoka la kushushwa ngazi, wakipigwa 1-0 nyumbani Sunderland.
Timu hiyo ilikuwa na nafasi ya kufungua pengo la alama tisa na West Ham ambayo ipo nambari 18 lakini wakakosa baada ya Habib Diarra kufungia Sunderland penalti ugani Elland Road.
Bao la Joe Rodon kwa Leeds liliondolewa kwa sababu alikuwa ameotea. Penalti iliyopewa Sunderland ilitokana na Ethan Ampadu kunawa mpira ndani ya kijisanduku.
Ushindi huo uliongeza alama za Sunderland hadi 40, alama 15 nje ya eneo hatari la kushushwa ngazi.
Brentford na Bournemouth ziliumiza nyasi bure, matokeo ambayo yalisongesha Bournemouth hadi nambari 10 huku Brentford ikiwa ya saba.