ODM katika hatari ya kupoteza Nairobi
CHAMA cha Orange Democratic Movement (ODM) kinakabiliwa na kazi ngumu kudumisha ubabe wake jijini Nairobi katika uchaguzi wa 2027 baada ya kifo cha kigogo Raila Odinga.
Tangu 2005 chama hicho cha chungwa kilipoanzishwa, Raila alihakikisha ODM inalemea vyama vingine huku akiwa mwaniaji wa urais aliyeshabikiwa sana na wakazi jiji kuu.
Katika kura ya 2017 ODM ilishinda kiti cha useneta, mbunge mwakilishi wa kike, viti 38 vya udiwani na viti vinane kati ya 17 vya ubunge.
Wabunge wa ODM Nairobi kwa sasa ni TJ Kajwang (Ruaraka), Phelix Odiwuor ‘Jalang’o’ (Langata), Peter Orero (Kibra), Anthony Oluoch (Mathare), Tim Wanyonyi (Westlands), Beatrice Elachi (Embakasi Kaskazini), George Aladwa (Makadara) na Babu Owino (Embakasi Mashariki).
Pia ni kupitia ODM ambapo Esther Passaris na Edwin Sifuna walishinda viti vya mbunge mwakilishi wa kike na seneta mtawalia.
Hata hivyo, baada ya kifo cha Raila chungwa inakabiliwa na kibarua moto hasa kufuatia mpasuko chamani ambapo sasa kuna mirengo miwili.
Mrengo wa kinara wa chama Dkt Oburu Oginga unatifuana na ule wa Linda Mwananchi unaoongozwa na Seneta Sifuna.
Hali kwamba ODM inaonekana kupata ugumu kudumisha umaarufu wake ilidhihirika wiki mbili zilizopita baada ya Wanyonyi kukutana na Dkt Oginga, ambapo aliombwa arejee jiji kuu ili kuwania kiti cha ugavana 2027.
Hata hivyo, Wanyonyi alikataa akisema ashakita siasa zake Bungoma huku duru zikiarifu kwamba pia ana makovu ya kupokonywa tikiti ya chama kuwania ugavana mnamo 2022.
Licha ya Wanyonyi kuonekana kuwa kifua mbele wakati huo, marehemu Raila alimshawishi atetee kiti chake cha ubunge huku Muungano wa Azimio ukimwasilisha Polycarp Igathe.
“Ni kweli Tim Wanyonyi alikutana na akina Dkt Oginga ambapo walijaribu kumshawishi arejee Nairobi kuwania ugavana, lakini akakataa. Aliwaambia kuwa ashaamua kupigania ugavana wa Bungoma na hata ashaanza kampeni,” alisema Mbunge wa Sirisia, John Waluke, ambaye ni mwandani wa Wanyonyi na anayeunga mkono azma yake ya 2027.
“Tim ameshaanza kampeni zake na ndiye kifua mbele katika kiny’ang’anyiro cha ugavana Bungoma. Hatuwezi kukubali arejee tena kuwania ugavana Nairobi,” akaongeza Waluke.
Mbunge huyo wa Westlands tayari amejitokeza hadharani na kutangaza kwamba anaegemea mrengo wa Linda Mwanachi wake Seneta Sifuna.
Ingawa hakuhudhuria mikutano ya Linda Mwananchi mjini Trans Nzoia na Bungoma majuma mawili yaliyopita, alituma wawakilishi wake na hata akatoa mabasi ya kusafirisha raia.
Mbunge wa Makadara George Aladwa ndiye sasa amejitokeza kusema analenga ugavana kupitia ODM, huku Babu Owino wa Linda Mwananchi akiwa tayari kasema hadharani awali kwamba hatatumia ODM kusaka kiti hicho.
Kumekuwa na wito gavana wa sasa Johnson Sakaja ajiunge na ODM ili kuwania ugavana kwa chama hicho, lakini Aladwa amesisitiza lazima kuwe na mchujo wa chama kupata mgombea halisi atakayetwaa tikiti hiyo.
Huku Passaris akiweka wazi kuwa hatatetea kiti chake cha mwakilishi wa kike, ODM haina mgombeaji mkakamavu katika nafasi hiyo.
Aliyekuwa Mwenyekiti wa Chama cha Mawakili Nchini (LSK) Faith Odhiambo ametangaza kusaka kiti hicho. Anaegemea Linda Mwananchi.
ODM pia inakabiliwa na migawanyiko ya ndani hasa katika mrengo wa Dkt Oginga.
Imebainika kuwa wasioridhika wataamua kuwania kama wagombeaji huru, na huenda wakabwagwa na wawaniaji wa vyama pinzani.
Kulingana na mchanganuzi wa masuala ya kisiasa Martin Andati, ODM kwa sasa imesalia kigae na isipobadili mikakati ushawishi wake katika jiji kuu utaisha.
“Raila alikuwa mjanja na mwenye mikakati, na hilo lilimsaidia kutawala siasa za jiji kwa miaka mingi. Jambo ambalo kwa sasa ni vigumu. Oburu hana ushawishi wowote kisiasa Nairobi. Wasipobadili mikakati chama kitapoteza sana 2027,” akasema mchanganuzi wa masuala ya siasa Martin Andati.
Anaonya kuwa ODM kwa sasa imesalia kigae na isipobadili mikakati uhai wake wa kisiasa jijini utaisha.
“Oburu hana ushawishi wowote kisiasa Nairobi. Unaona hata hana wagombeaji maarufu wa ugavana, mbunge mwakilishi wa kike na useneta. Viongozi wengi maarufu wako mrengo wa Linda Mwananchi. Kwa hivyo wasipobadili mikakati chama kitapoteza sana uwakilishi 2027,” akaeleza.