Wagonjwa waendelea kuteseka mgomo wa wauguzi ukikosa suluhu mpaka sasa
WAGONJWA kote nchini wanaendelea kuteseka huku mgomo wa wahudumu wa afya ukiendelea bila suluhu, hali ambayo imelemaza utoaji huduma katika hospitali nyingi za umma.
Baraza la Magavana (CoG) linasisitiza kuwa wahudumu hao wanapaswa kurejea kazini kwa kuwa mchakato wa kushughulikia malalamishi yao tayari umeanza.
Hata hivyo, viongozi wa vyama vya wafanyakazi wa sekta ya afya wanashikilia kuwa mgomo huo hautasitishwa hadi matakwa yao yote yatimizwe kikamilifu.
Akizungumza katika mdahalo wa vyombo vya habari Jumanne, Mkurugenzi Mkuu wa Baraza la Magavana Mary Mwiti alisema mzozo huo unatarajiwa kutatuliwa kabla ya mwisho wa wiki.
“Ni sehemu tu ya wahudumu wa afya walio katika mgomo. Tukilinganisha hali ilivyo sasa na kabla ya ugatuzi, tuko katika nafasi bora zaidi,” alisema.
Aliongeza kuwa migogoro ya wafanyakazi wa afya imepungua kwa kiasi kikubwa katika kipindi cha miaka saba iliyopita.
Ingawa Bi Mwiti alisema ni makundi mawili pekee ya wahudumu yaliyo katika mgomo, imebainika kuwa makundi mengine kadhaa pia yamesusia kazi, yakiwemo maafisa wa afya ya umma, wauguzi, maafisa wa utabibu, wafamasia na maafisa wa maabara.
Kuhusu maafisa wa utabibu, alisema Baraza la Magavana tayari limekubaliana kuhusu Mkataba wa Pamoja (CBA) na kuutia saini. Pia alisema mfumo wa kurejea kazini umekamilishwa, lakini utekelezaji wake unahitaji kufuata taratibu fulani.
Alifafanua kwamba baada ya CBA na makubaliano ya kurejea kazini kutiwa saini, Tume ya Mishahara na Marupurupu (SRC) lazima ithibitishe mishahara na marupurupu mapya ili viwango viwe sawa katika makundi mbalimbali ya watumishi.
Bi Mwiti alisema magavana walikutana Alhamisi iliyopita kujadili masuala yanayowahusu wauguzi na kukubaliana kuhusu hatua mbalimbali za kuwawezesha kurejea kazini. Aliongeza kuwa kutakuwa na mkutano mwingine wa kukamilisha mazungumzo hayo.
“Tunangoja kupokea barua rasmi na Baraza la Magavana liko tayari kushiriki mazungumzo ili kurejesha kikamilifu huduma kwa wananchi,” alisema.
Serikali pia inatarajiwa kufanya Mkutano Mkuu wa Kitaifa wa Afya wa siku mbili wiki ijayo ambapo suala la wahudumu katika sekta ya afya litajadiliwa.
“Ninaamini kabla ya mwisho wa wiki tutakuwa tumekubaliana. Kufikia wakati wa mkutano huo, migomo yote itakuwa imekwisha,” alisema.
Hata hivyo, mwenyekiti wa chama cha maafisa wa utabibu Kenya Peterson Wachira alisema SRC tayari imetekeleza wajibu wake kwa kutoa mwongozo wa utekelezaji wa mishahara mipya.
“Sasa tunasubiri Baraza la Magavana kufanya marekebisho ya mishahara katika mfumo wa malipo. Wanapaswa kuwasiliana na Wizara ya Utumishi wa Umma ili hatua hiyo ikamilike,” alisema.
Wachira alisema kumekuwa na maendeleo katika kutiwa saini kwa makubaliano ya kurejea kazini katika kaunti nyingi, lakini kaunti 18 bado hazijakamilisha mchakato huo. Kaunti hizo ni pamoja na Kisumu, Kakamega, Busia, Kajiado, Uasin Gishu, Nyandarua, Embu, Kiambu, Nyeri na Murang’a.
“Natarajia kukamilisha hatua zote wiki ijayo. Kufikia sasa hakuna jambo la msingi lililotoka kwenye mikutano tuliyofanya. Tutakutana tena na Baraza la Magavana Alhamisi kujadili masuala yetu,” alisema.
Katibu Mkuu wa Muungano wa Wataalamu wa Afya ya Mazingira na Afya ya Umma Kenya (KEHPHPU), Brown Ashira, alisema hakuna hata takwa moja la wanachama wao ambalo limetekelezwa.
“Magavana bado wanataka turejee kazini bila makubaliano yoyote,” alisema.
Aliongeza kuwa huduma muhimu kama chanjo zimeathirika huku kukiwa na ongezeko la magonjwa yanayosababishwa na chakula na maji yasiyo salama.
Kwa upande wake, Naibu Katibu Mkuu wa Muungano wa Kitaifa wa Wauguzi Kenya Lucy Mburu, alisema bado hawajafikia muafaka katika mazungumzo yao na Baraza la Magavana.
“Tumekutana na mpatanishi kutoka Wizara ya Kazi lakini bado hakuna makubaliano. Tutakuwa na mkutano mwingine wiki ijayo,” alisema.