Ndio, unaweza kujitawadha bila maji! Huu hapa ufafanuzi kamili…
JE, wajua kuwa endapo maji yatakosekana, Uislamu unaruhusu waumini kutumia udongo, mchanga, mawe au vumbi safi maarufu kujisafisha kabla kusali?
Katibu Mkuu wa Baraza la Maimamu na Wahubiri wa Kiislamu nchini (CIPK) tawi la Lamu, Sheikh Mohamed Abdulkadir, anataja hali tatu zinazoruhusu Muislamu kufanya hivyo, maarufu kama ‘tayamamu’.
Mojawapo ni ikiwa maji hayapatikani kabisa, hayawezi kutumika au hayatoshi kwa udhu.
Pili, Muislamu hutekeleza tayamamu endapo ni mgonjwa, anaumwa, hivyo matumizi ya maji huenda yakamdhuru au hata kuchelewesha kupona kwake.
“Njia ya tatu ni endapo kuna haja ya kuokoa maisha, iwe ni ya binadamu au hayawani anayeumia kwa kiu. Ikiwa kukosa maji hayo kutamfanya apoteze uhai basi ni vyema kuokoa maisha kwa kwa kupeana maji hayo yanywewe badala ya kuyatumia kutawadhia,” akasema Bw Abdulkadir.
Kiongozi wa dini kisiwani Lamu, Bw Mahmoud Abdulkadir, pia alitaja hali endapo kuna baridi kali na maji hayawezi kupashwa moto.
“Pia endapo maji hayo yapo lakini ni mbali sana au kuna hatari ya kuyapata yalipo, basi mja anaweza kutumia udongo safi, mchanga au mawe kujisafisha,” akasema Bw Ahmed.
Kiongozi wa Msikiti wa Kibarani, Kaunti ya Kilifi, Ustadh Hassan Khalfan alieleza taratibu zifaazo.
Anasema ni vyema mtu kusema Bismillah kabla ya kupiga viganja vya mikono yote miwili kwenye udongo safi, mchanga au mawe.
“Utastahili kupuliza viganja kuondoa vumbi lililozidi. Kisha utumie vumbi hilo kupaka uso mzima kwa viganja hivyo mara moja. Pia unapaswa kupaka mkono wa kulia kwa kutumia kiganja cha kushoto mpaka kwenye kiwiko. Kadhalika fanya vivyo hivyo kwa mkono wa kushoto,” akasema Bw Khalfan.
Naye Kiongozi wa Msikiti wa Jamia ulioko Mokowe, Ustadh Ali Bwanamkuu anaitaja tayamamu kuwa ishara ya njia rahisi katika Uislamu, kama inavyoelezwa na Mwenyezi Mungu ambaye kamwe hataki kufanya ugumu kwa watu kujitawadha bali kuwarahisishia kwa ajili ya ibada au kuswali.