Mhubiri kicheche aanikwa sokoni kwa hadaa ya sadaka
KAILU, MACHAKOS
KULIZUKA kioja katika mtaa huu baada ya jamaa aliyekuwa akijifanya mhubiri kuanikwa hadharani na kuambiwa aache ujanja wa kuomba sadaka kwa njia ya hila.
Jamaa huyo alikuwa akizunguka mitaani na hata kupenya katika mabanda ya biashara akijitambulisha kama pasta kutoka kanisa lisilojulikana.
Kwa sauti ya kuigiza unyenyekevu, aliwahubiria wakazi kuhusu baraka na miujiza kisha kuwahimiza watoe sadaka ili “kazi ya Mungu isonge mbele.”
Hata hivyo, wakazi walianza kumtilia shaka walipogundua hana kanisa maalum wala ushahidi wowote wa wito wake.
Uchunguzi ulionyesha kuwa hana hata Biblia yake binafsi bali huazima kila anapohitaji kuhubiri.
Siku ya aibu ilifika alipokabiliwa na baadhi ya wakazi waliomtaka ataje kanisa lake na viongozi wenzake.
Aliposhindwa kujibu maswali rahisi, alizomwa na kuambiwa aache kuwahadaa watu kwa jina la dini.
Wakazi walimshauri atafute kazi ya kufanya badala ya kujifanya pasta ili apewe sadaka huku mjadala ukiibuka kuhusu matapeli wanaotumia dini.