Mbegu za kiume zinatungisha mimba msimu wa joto kuliko wa baridi – Utafiti
WATAFITI wamebaini kuwa msimu wa joto ndio wanawake hushika mimba kwa urahisi kutokana na ubora na urahisi wa mbegu za kiume kutoka sehemu moja hadi nyingine kukutana na zile za kike.
Utafiti huo ulifanywa na wanasayansi kutoka vyuo vikuu vinavyopatikana Canada, Uingereza na Denmark baada ya kutathmini sampuli za shahawa zilizokusanywa kati ya 2018 na 2024 kutoka kwa wanaume 15,000.
Wanaume hao walikuwa wamejitolea kuchangia mbegu zao za kiume kwa kliniki mbalimbali Denmark na Florida.
Wakati wa utafiti huo, watafiti walizingatia kiwango cha shahawa, mbegu za kiume ndani yake na jinsi mbegu zenyewe zinaweza kuogolea ndani ya mshahawa kisha kusonga mbele na kukutana na zile za kike.
Wingi wa mbegu za kiume pamoja na kiwango cha mbegu za kiume hazikuathirika kutokana na msimu au kubadilika kwa hali ya hewa kwa mujibu wa utafiti huo.
Hata hivyo, kasi ya uogoleaji wa mbegu za kiume ndani ya mshahawa nayo ilibadilika.
Kaskazini na Kusini mwa Amerika, mbegu za kiume zilikuwa zikisonga kwa kasi zaidi kati ya Juni na Julai ambayo ni msimu wa joto.
Kasi hiyo hata hivyo ilikuwa chini kati ya Desemba na Januari ambayo ni msimu wa baridi kali.
“Tulishangazwa na jinsi tofauti ya msimu ilichangia kubadilika kwa kasi ya mbegu za kiume. Hata Florida ambako kuna joto, bado mbegu za kiume zilikuwa zikiogolea kwa kasi lakini ikifika msimu wa baridi, kasi hiyo ilikuwa chini,” akasema Mtaalamu Allan Pacy ambaye ni kati ya wataalamu wa afya walioshiriki utafiti huo.
Matokeo ya utafiti huo hata hivyo hayakuonyesha iwapo mtindo wa maisha kama mabadiliko ya mazingira yanachangia pia tofauti kwenye kasi ya mbegu za kiume.
Utafiti huu sasa unaenda kinyume na zile za awali ambazo zimekuwa zikionyesha kuwa msimu wa baridi ndio uwezekano wa kushika mimba upo juu kuliko msimu wa joto.