Afya na Jamii

Wataalam waelezea hofu ya kaswende kukosa kugunduliwa mapema kwa wanawake

Na MARY WANGARI June 11th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

MAAMBUKIZI ya kaswende kwa wanawake yameongezeka pakubwa katika kipindi cha mwongo mmoja uliopita, huku wataalam wakionya kuwa gonjwa hilo huenda linaachwa bila kugunduliwa kwa sababu dalili zake hukosa kugundulika kirahisi.

Kwa mujibu wa wataalam, visa vingi vya wanawake husalia bila kugunduliwa kwa sababu dalili za maambukizi ni finyu na aghalabu hudhaniwa kuwa za matatizo ya kawaida zaidi kiafya.

Dalili za mwanzo za kaswende zinazojumuisha vidonda visivyo na uchungu, aghalabu hujitokeza kwa ndani au katika maeneo yasiyo rahisi kuonekana kumaanisha hukaa bila kuonekana, wataalam wanasema.

Mwanamke aliye na tatizo la mwasho kwenye sehemu za siri. Picha|Maktaba

Hata zinapoonekana, dalili hizo za vidonda hudhaniwa kuwa maradhi ya tutuko, kandidiasi, vinywele vinavyootea kutoka ndani na matatizo madogomadogo ya ngozi.

Si ajabu kaswende hufahamika kama “mwigizaji mahiri” kwa sababu inaweza kujifananisha na aina anuai ya maradhi mengineyo.

Kaswende inapozidi kukolea, upele hujitokeza kwenye viganja vya mikono na miguu, hali inayoweza kuchukuliwa kuwa aina tofauti za ugonjwa wa ngozi au mzio.

Wanasayansi kutoka Taasisi za Matibabu za Brighton na Sussex wamegundua ucheleweshaji katika ugunduzi baada ya kutathmini visa kadhaa.

Katika udadisi wao ulioshirikisha wagonjwa sita, walithibitisha visa kadhaa vya fursa zilizokosa kubainika za kupima kaswende hata baada ya washiriki kuwasilisha dalili sugu ikiwemo vijipu vyenye usaha, maumivu na uvimbe kwenye nyonga.

Kupoteza uwezo wa kusikia, uharibifu wa neva na ini kufanya kazi kwa njia isiyo ya kawaida ni miongoni mwa dalili hizo sugu.

Kutokana na hali hiyo, wataalam wanasema baadhi ya wagonjwa walipitia vipimo visivyohitajika na wakati mwingine vya kuwaingilia zaidi, huku wengine “wakiathirika pakubwa kisaikolojia.”

“Maambukizi mengi yanaweza kusalia bila dalili thabiti huku yakizidi kuathiri mwili. Kufikia wakati baadhi ya watu wanagunduliwa kuugua kaswende, huenda tayari wanakabiliwa na matatizo yanayohusiana na nguvu za uzazi au athari za muda mrefu zinazohusu afya ya uzazi,” anafafanua Valentina Milanova, Mkurugenzi wa Kampuni ya Afya ya Wanawake kwa jina Daye.

Anasema unyanyapaa na dhana potovu zinazozingira vipimo vya kaswende zinachangia wagonjwa kukosa kupimwa.

“Bado kuna dhana kuwa vipimo vya maradhi ya zinaa vinahitajika tu kwa makundi au tabia fulani – lakini hilo si kweli. Afya ya kujamiiana inapaswa kuchukuliwa kama huduma nyingine yoyote ya kawaida kuhusu afya.”

Alisema inahofisha jinsi mfumo wa afya unakabili vipimo vya maradhi ya zinaa.

“Aghalabu husawiriwa kama kitu wanachofanya watu baada ya kugutushwa, badala ya sehemu ya kawaida ya huduma ya afya ya kinga.”