Serikali kupeana sehemu za Bandari ya Mombasa, Lamu zisimamiwe na watu binafsi
SERIKALI iko katika hatua ya mwisho ya kuwezesha sehemu za Bandari ya Mombasa na Lamu kusimamiwa na mashirika ya kibinafsi.
Serikali imenuia kufuta Sheria ya Mamlaka ya Bandari ya Kenya (KPA) ili kuondoa mamlaka hiyo na kuibadilisha kuwa Kampuni ya Umma yenye Hati ya Hisa (PLC) chini ya Sheria ya Kampuni.
Hii itarahisisha uwekezaji wa sehemu ya Bandari ya Mombasa na gati tatu za Bandari ya Lamu.
Kwenye hati ya Mwisho ya Uwazi wa Ushirikiano wa Umma na Sekta Binafsi (PPP) katika Sekta ya Bandari ya Kenya, imebainika serikali inalenga kuongeza mapato ya bandari za Mombasa na Lamu kwa Sh44 bilioni kila mwaka.
Serikali inasema kwamba Sheria ya Mashirika Yanayomilikiwa na Serikali (GOE) iliyopitishwa Novemba mwaka jana inatoa nafasi kwa KPA kuhamia kwenye mfumo wa kampuni binafsi.
“Sheria ya GOE italazimisha KPA kuwa na faida na kujitegemea. Miundo ya PPP ndiyo njia bora ya kufanikisha malengo haya. Mara tu KPA ikipata hadhi ya GOE, mamlaka itatarajiwa kufanya kazi kama shirika la kibiashara linalolenga faida,” hati hiyo imeeleza.
Chini ya mfumo uliopendekezwa, shughuli za mizigo zitapelekwa kwa sekta binafsi kwa muda. Kwa kuwa na haki ya kufanya kazi hiyo, kampuni binafsi italipa KPA ada ya leseni.
Imeelezwa wazi kuwa, hakuna miundomsingi ya umma inayouzwa, na serikali bado itashikilia mamlaka ya kudhibiti.
Bandari nyingine duniani zinazofanya kazi kwa mfumo huu ni pamoja na Los Angeles, New York, Hamburg, Rotterdam, Tanger, Santos, Singapore, na nyinginezo.
Katika mahojiano ya hivi majuzi, Waziri wa Barabara na Usafirishaji, Bw Davis Chirchir, alisema Sheria ya GOE, iliyopitishwa Novemba 21, 2025, na kuanza kutumika Desemba 2025, inabadilisha mashirika ya umma, ikiwemo KPA, kuwa mashirika ya kibiashara, yenye kujitegemea chini ya Sheria ya Kampuni.
“GOE itakuwa mabadiliko makubwa kuifanya KPA ifanye kazi kama sekta binafsi. Sheria hii inalenga kusawazisha uongozi wa mashirika ya umma kwa kutenga sera na usimamizi wa kila siku, kuimarisha uwajibikaji na kurahisisha maamuzi,” alisema Waziri.
Kwenye mpango huu, kampuni binafsi inatarajiwa kutengeneza upya gati ya 11 hadi 14 za Bandari ya Mombasa, ambazo zinahitaji ukarabati haraka kwa gharama ya Sh45 bilioni.
Bandari ya Lamu haijafikia uwezo wake wa kibiashara, ikifanya kazi kwa asilimia tano tu ya uwezo wake. Ushirikiano na sekta binafsi unaweza kuongeza ukuaji wa kibiashara wa bandari na kupunguza mzigo wa kifedha kwa serikali.
Hata hivyo, wadau kadhaa wamesalia na maswali kuhusu hatma ya maelfu ya wafanyakazi, kwani kampuni itafanya kazi na idadi ndogo ya wafanyakazi.
Mkurugenzi Mtendaji wa Shippers Council of Eastern Africa (SCEA), Bw Agayo Ogambi, alisema jambo muhimu ni kuwa, PPP hizi zifanywe kwa uwazi, kuhakikisha maslahi ya umma na taifa yamezingatiwa.
“Kitu muhimu ni usalama wa ajira. Bandari hii inatoa riziki kwa mamilioni, na kupotea kwa ajira kunaweza kuwa na madhara makubwa,” alisema.
Mchanganuzi wa masuala ya ubaharia, Bw Andrew Mwangura, alisema kupelekwa kwa Bandari ya Lamu kwa sekta binafsi kutasaidia kuboresha biashara, lakini usimamizi wa wafanyakazi lazima ufanywe kulingana na sheria za leba.
Hati iliyochapishwa inatoa chaguo kadhaa kwa wafanyakazi, ikiwa ni pamoja na kupelekwa kwenye mashirika mengine ya serikali.
Serikali pia inatoa chaguo kwa wafanyakazi kuendelea au kuacha kazi, kulingana na sheria za leba na matokeo ya ushauri yaliyoafikiwa.