Aga Khan yauza hisa zake za Nation Media Group kwa Taarifa Limited ya Tanzania
SHIRIKA la Maendeleo la Aga Khan (AKFED), jana lilitangaza kuuza hisa zake za Kampuni ya Habari ya NMG kwa Taarifa Limited inayomilikiwa na Bw Rostam Azizi, mfanyabiashara Tanzania.
Bw Azizi ana biashara nyingi katika sekta mbalimbali ikiwemo habari, uchimbaji madini, kilimo, ujenzi miongoni mwa nyingine.
Shirika hilo la Aga Khan, lilisema kwenye taarifa kwamba limeingia kwenye makubaliano ya kuuza hisa zake zote kwa Taarifa Limited. Aga Khan ilikuwa inamiliki asilimia 54.08 katika Nation Media, kwa maana hiyo ilikuwa mmiliki mwenye usemi mkubwa katika kuendesha biashara hiyo ya habari.
Kununuliwa huko kunamaanisha kwamba usimamizi wa Aga Khan katika kampuni hii ya habari ambao umedumu kwa miaka 66 sasa umetamatika, hivyo kuiweka NMG katika mikono ya Taarifa Limited.
Aga Khan ilianzisha Nation Media mnamo 1959.
“NMG sasa imejiweka pazuri kuimarisha uwezo wake kwa kuwekeza zaidi katika mabadiliko ya kidijitali. Taarifa Limited imejitolea kufanikisha mabadiliko haya na kusaidia shirika kuboresha uhusiano wake na wateja na kuendeleza tamaduni yake ya miaka mingi ya uanahabari unaoshughulikia maslahi ya mwananchi,” ikasema taarifa ya pamoja ya Akfed na Taarifa Limited.
Mchakato wa kubadilishana umiliki huo unatarajiwa kukamilika ndani ya muda wa miezi minne baada ya kutimiza masharti yote ya uidhinishaji.
Taarifa Ltd ilithibitisha kuwa haina mpango wa kununua hisa zilizosalia za NMG. Hisa za NMG zimeorodheshwa kwenye soko la Hisa la Nairobi pamoja na Uganda, Dar es Salaam na Rwanda.
Muadhama Aga Khan IV alianzisha NMG akiwa na maono ya kuwa na chombo huru cha habari ambacho kilisaidia kupanua mawanda ya uongozi wa kidemokrasia wakati taifa lilipojinyakulia uhuru.
NMG ilianza kwa kuchapisha Gazeti la Taifa Leo ambalo lililenga kuwapa Waafrika sauti nyakati za kupigania uhuru.
Kwa muda wa miaka 60 iliyopita, NMG imekuwa na sasa ina zaidi ya brandi 30 katika mataifa manne ambapo inawafikia zaidi watumiaji wa mitandao milioni 62.
Pia imetoa nafasi za ajira kwa zaidi ya watalaamu 1,000 katika ukanda huu.
Gazeti la Daily Nation nalo lilichapishwa kwa mara ya kwanza mnamo Machi 20, 1960.
NMG ilikuwa kati ya vyombo vya habari vya kwanza kuorodheshwa kwenye soko la hisa na imekuwa ikifanyia biashara hisa zake sokoni humo tangu 1973.
Katika historia yake nzima, kampuni hii imedhihirisha maadili katika utendakazi wake.
Bw Azizi, ambaye sasa ndiye mmiliki wa hisa nyingi katika NMG, ni mfanyabiashara maarufu aliye na kampuni nyingi Afrika Mashariki. Alihusika katika kuzindua magazeti ya Mwananchi, The Citizen ambayo yalinunuliwa baadaye na NMG. Kwa sasa, anashikilia umiliki katika Habari Corporation, ambalo ni shirika la habari Tanzania.
“Tumeheshimishwa sana kuibuka wenyehisa wakuu wa Nation Media Group,” akasema Bw Azizi. “NMG ni shirika la umuhimu mkubwa Afrika Mashariki na tutaendeleza uhuru wa uanahabari huku tukiwekeza katika ufanisi wake kama shirika lisiloegemea upande wowote kwenye kanda hii.”
Afisa Mkuu Mtendaji wa Nation Media Group Geoffrey Odundo alisema shughuli za kampuni zitaendelea kama kawaida. Bodi na usimamizi utaendelea kusimamia shughuli zote za uanahabari wa kuaminika unaotumikia jamii,” akasema Bw Odundo.