Habari za Kitaifa

Madereva wapumua mahakama ikizima NTSA kuwatoza faini za papo hapo

Na RICHARD MUNGUTI March 13th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

WENYE magari na madereva wamepata afueni baada ya Mahakama Kuu ya Milimani kusitisha kwa muda mfumo wa faini ulioanzishwa na Mamlaka ya Kitaifa ya Usalama na Uchukuzi (NTSA).

Uamuzi huu ulifuatia kesi iliyowasilishwa na kundi la haki za binadamu, Sheria Mtaani kupitia kwa Bw Shadrack Wambui.

Jaji wa Mahakama Kuu, alifahamishwa kuwa NTSA haikufuata masharti ya ushirikishaji wa umma kabla ya kuanzisha mfumo huu.

Aidha, walalamishi wanadai kuwa NTSA ilitwaa mamlaka ya Mahakama na Ofisi ya Mkurugenzi wa Mashtaka ya Umma (DPP) kwa kuendesha kesi kinyume cha sheria na kutoza faini bila taratibu za kisheria.

Sheria Mtaani ilieleza mahakamani kuwa faini zinazokusanywa zinapelekwa katika akaunti katika benki ya KCB ambayo inamilikiwa na watu wasiojulikana, na akaunti hiyo haiendeshwi na Mahakama.

Wakili wa Sheria Mtaani, Danstan Omari, aliomba mahakama kuingilia kati na kulinda haki za raia dhidi ya shughuli zisizo halali za NTSA.

Aidha, mahakama ilisikiliza madai kuwa NTSA inafanya kazi kama mahakama kinyume cha sheria, bila majaji au waendesha mashtaka, na kwamba madereva na wenye magari wanaadhibiwa bila kupatiwa haki ya kusikizwa.

Vilevile, wadau wengine wakiwemo Constantine Okello Ofula na Kennedy Maingi Mutwiri, walipinga hatua na NTSA wakidai inakiuka haki za kikatiba za wananchi.

Mahakama ilizuia NTSA, Mwanasheria Mkuu, na KCB kuendeleza mfumo huo wa faini hadi kesi hiyo itakaposikilizwa na kuamuliwa.

“Hadi kesi itakaposikilizwa, maagizo ya muda yanatolewa kuzuia washtakiwa kutekeleza faini hizi,” alisema jaji.

Kesi ililenga mfumo wa kamera za trafiki zinazotumika kugundua ukiukaji wa sheria barabarani na kutuma faini kupitia ujumbe mfupi wa simu (SMS).

Walalamishi hao wanasema mfumo huu hauna msingi wa kisheria na unakiuka kanuni za haki ya kikatiba, ikiwemo dhana ya kutokuwa na hatia na haki ya kusikilizwa katika mahakama.

Walalamishi wanasema kuwa ukiukaji wa sheria za trafiki lazima ushughulikiwe mahakamani, ambapo mtu ana nafasi ya kujitetea na kupinga ushahidi kabla ya kuadhibiwa.

Mahakama imewaagiza walalamishi kukabidhi washtakiwa stakabadhi za kesi kufikia leo Machi 13, 2026, na NTSA iwasilishe majibu kufikia Machi 20.

Kesi itatajwa tena Aprili 9, 2026.