Hofu visa vya watu kujitia kitanzi Naivasha vikizidi
ENEO la Naivasha limekumbwa na mlipuko wa visa vya watu kujitia kitanzi, huku vifo vikitishia ustawi wa familia na jamii.
Kati ya Mei 2025 na Machi 3, 2026 na angalau watu 50 wamefariki kwa kujitoa uhai wengi wakiwa wanaume, kutokana na matatizo ya kifamilia, hasira, na changamoto za kiuchumi.
Tukio la hivi karibuni lilihusisha mwanaume wa miaka 35 katika mtaa wa Mithuri. Wakati wa tukio hilo, majirani walimsikia akilalamika kuhusu hali ngumu ya kiuchumi.
Visa kama hicho vimekuwa vikitokea mara kwa mara, hasa kwa walinzi wa usiku wanaojitoa uhai baada ya kufutwa kazi kutokana na hatua za kampuni za maua za kupunguza gharama.
Wakazi wa eneo hilo wanasema vifo vingi vinahusiana na matatizo ya kiuchumi, migogoro ya kifamilia, matumizi ya dawa za kulevya, na changamoto za mahusiano.
Katika visa vingi, wafanyakazi wa kampuni za maua ndio wanaokumbwa na hali hii, wakiwa na msongo wa mawazo kwa kupoteza ajira zao.
Shirika la Naivasha Gender-Based Violence (GBV) Cluster Group, linasema kuwa watoto wadogo pia wameathirika.
Kwa mfano, mvulana wa miaka 10 alijitia kitanzi eneo la Ndabibi kabla ya shule kufunguliwa, huku mwanafunzi wa kidato cha pili akifariki kwa kujitoa uhai nje ya nyumba ya wazazi wake aliposimamishwa kuhudhuria shuleni.
Lydia Ng’ang’a, mratibu wa afya ya akili wa Kaunti ya Nakuru, alisema ongezeko la visa hivi linatokana na msongo wa mawazo, wasiwasi, na uraibu wa dawa za kulevya.
“Matatizo ya akili ndiyo sababu kubwa inayosukuma watu kuamua kujitoa uhai. Pia matatizo ya mahusiano, changamoto za kijamii na kiuchumi, pamoja na historia ya familia ya kujitia uhai ni sababu nyingine,” alisema.
Viongozi wa dini, polisi, na wasimamizi wa jamii wanasema matatizo ya kifamilia, madeni, migogoro ya ndoa, uraibu wa dawa na pombe, na hali ngumu za kiuchumi vinachangia tatizo hili.
Mwanasaikolojia James Mwaura, alisema matatizo ya kifamilia, umasikini na uraibu vinachangia kwa kiasi kikubwa.
Askofu John Kariuki alisema ukosefu wa mwongozo wa wazazi na usimamizi mbaya wa hasira pia zinachangia visa vya watu kujitoa uhai.
Kaimu Mkuu wa Polisi wa Naivasha Anthony Keter, alisema visa hivi vinatokana hasa na hali ngumu ya maisha na migogoro ya kifamilia.
Wengine, hasa vijana waliokuwa wafanyakazi wa kampuni za maua, wanapoteza matumaini baada ya kupoteza ajira zao, hali inayosababisha baadhi yao kujitia kitanzi.
Mkuu wa idara ya afya ya akili Kaunti ya Nakuru, Ms Ng’ang’a, alisisitiza umuhimu wa jamii kutafuta msaada wa kitaalamu au kutoka kwa familia na marafiki.