Kimataifa

Kisasi: Trump atishia kulipua kituo cha mafuta cha Iran mashambulizi yakichacha

Na MASHIRIKA March 15th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS wa Amerika Donald Trump ametishia kuishambulia miundombinu ya mafuta ya Iran katika kisiwa cha Kharg iwapo Tehran haitaacha kushambulia meli katika Mkondo wa Hormuz, hatua inayoweza kuongeza misukosuko katika soko la mafuta duniani.

Trump alitoa onyo hilo Ijumaa kupitia mitandao ya kijamii akisema kuwa Amerika tayari “imeharibu kabisa” malengo ya kijeshi kwenye kisiwa hicho, ambacho ndicho kituo kikuu cha kusafirisha takriban asilimia 90 ya mafuta ya Iran kwenda nje ya nchi.

Hata hivyo, alisema mashambulizi ya Amerika hayakulenga miundombinu ya mafuta ya Kharg.
Alionya kuwa ikiwa Iran au upande mwingine wowote utaingilia usalama wa meli za kusafirisha mafuta katika Mkondo wa Hormuz, ataweza kubadili uamuzi huo mara moja.

Trump alisema Iran haina uwezo wa kujilinda dhidi ya mashambulizi ya Amerika.

Kupitia jukwaa lake la Truth Social, aliandika kuwa wanajeshi wa Iran na washirika wao wanapaswa kujisalimisha ili kuokoa kile kilichobaki cha nchi yao.

Hata hivyo, Iran haijaonyesha dalili zozote za kukubali shinikizo za kijeshi kutoka Amerika na Israel.

Jeshi la Iran lilisema kuwa shambulio lolote dhidi ya miundombinu yake ya mafuta au nishati litajibiwa kwa mashambulizi dhidi ya vituo vya kampuni za mafuta zinazoshirikiana na Amerika katika eneo hilo.

Shirika la habari la Iran Fars liliripoti kuwa zaidi ya milipuko 15 ilisikika katika kisiwa cha Kharg wakati wa mashambulizi ya Amerika.

Vyanzo vilisema mifumo ya ulinzi wa anga, kambi ya wanamaji na miundombinu ya uwanja wa ndege ilishambuliwa, lakini miundombinu ya mafuta haikuathiriwa.

Wakati huo huo, masoko ya kimataifa yanaendelea kufuatilia kwa karibu iwapo mashambulizi hayo yameharibu mtandao wa mabomba, vituo vya kuhifadhia mafuta na matangi katika kisiwa hicho, kwani hata usumbufu mdogo unaweza kupunguza zaidi usambazaji wa mafuta duniani.

Iran pia ilidai kuwa imefanikiwa kuangusha droni tano katika anga yake, na kufanya jumla ya droni za Amerika na Israeli ilizodungua tangu vita kuanza kufikia 114.

Vita hivyo vilianza Februari 28 baada ya mashambulizi makubwa ya Amerika na Israeli dhidi ya Iran, na sasa inakuwa mzozo wa kikanda ulio na athari kubwa kwa masoko ya nishati na uchumi wa dunia.

Kwa mujibu wa jeshi la Israeli, zaidi ya maeneo 200 yameshambuliwa katika magharibi na katikati mwa Iran katika kipindi cha saa 24 zilizopita, vikiwemo vituo vya kurushia makombora ya masafa marefu, mifumo ya ulinzi wa anga na viwanda vya silaha.

Baada ya wiki mbili za vita, zaidi ya watu 2,000 wameuawa, wengi wao nchini Iran lakini pia nchini Lebanon na katika mataifa ya Ghuba.

Mamilioni ya watu wamelazimika kuhama makazi yao kutokana na mapigano hayo.

Iran pia imejaribu kuvuruga usafirishaji wa mafuta kupitia Mkondo wa Hormuz, njia muhimu inayopitisha takriban asilimia 20 ya nishati ya mafuta duniani.

Amerika imesema hivi karibuni jeshi lake la wanamaji litaanza kusindikiza meli za mafuta ili kuhakikisha usalama wa usafiri katika njia hiyo muhimu ya bahari.