Kimataifa

Trump ataka mataifa rafiki yamsaidie kupambana na Iran

Na REUTERS March 16th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

FLORIDA, AMERIKA

RAIS Donald Trump ameyaagiza mataifa rafiki yanayopokea mafuta kupitia Mkondo wa Hormuz kusaidia kuhakikisha usafirishaji wa mafuta katika mkondo huo muhimu wa bahari unaendelea bila vikwazo, akiyahimiza kutuma meli za kivita kuimarisha usalama katika ‘njia’ hiyo ya kimataifa.

Trump alisema Amerika iko tayari kushirikiana na mataifa hayo ili kuhakikisha usafirishaji wa kawi unafanyika “upesi, kwa njia laini na bora”.

Agizo hilo linajiri huku mvutano kati ya Amerika-Israel na Iran ukiendelea kuongezeka, baada ya Tehran kutishia kusitisha usafirishaji wa mafuta kupitia mkondo huo ambao hupitisha takribani asilimia 20 ya mafuta yote duniani.

Mkondo wa Hormuz ni njia muhimu ya usafirishaji wa mafuta kimataifa na hatua yoyote ya kuufunga inaweza kuvuruga pakubwa soko la nishati duniani.

Nchi za dunia zinazopokea mafuta kupitia Mkondo wa Hormuz ni sharti zishughulikie mkondo huo, na tutasaidia – Pakubwa!” Trumo aliandika kwenye mtandao wa kijamii Jumamosi.

“Amerika itashirikiana na mataifa hayo ili kila jambo lifanyike upesi, kwa njia laini na bora.”

Matamshi hayo yaliashiria mabadiliko makubwa kutoka kwa Trump ambaye awali alisema Amerika inalenga vituo vya kijeshi pekee vilivyopo Kharg, na kudidimiza juhudi za kidiplomasia.

Serikali yake imepuuzilia mbali juhudi za wandani wa Mashariki ya Kati kuanzisha majadiliano, duru zilieleza Reuters.
Trump kupitia ujumbe kwenye mtandao wake wa kijamii, Truth Social, alirai China, Ufaransa, Japan, Korea Kusini, Uingereza na mataifa mengine kutuma meli za kivita kwenye Mkondo wa Hormuz.

Hakuna taifa lolote liliashiria papo hapo kwamba litafanya hivyo.

Takayuki Kobayashi, mkuu wa sera za chama tawala Japan, alikataa kukanusha uwezekano huo lakini akaaleza idhaa ya taifa hilo, NHK kuwa “kiwango cha kisheria ni cha juu mno.”

Japan hutafsiri katiba yake iliyobuniwa baada ya vita kumaanisha inaweza kutuma jeshi lake ikiwa ustawi wa taifa hilo unatishiwa.

Ufaransa inajitahidi kukusanya muungano kuimarisha usalama katika Mkondo wa Hormuz mara tu hali ya usalama itakaporejea, huku Uingereza ikijadili mbinu mbalimbali na wandani wake kuhakikisha usalama wa usafirishaji, maafisa wamesema.

Kiongozi wa Kidini Iran, Ayatollah Mojtaba Khamenei, aliyemrithi baba yake aliyeuawa, amesema Mkondo wa Hormuz ufungwe.

Waziri wa Masuala ya Kigeni, Iran, Abbas Araqchi alisema Iran itajibu mashambulizi yoyote dhidi ya vituo vyake vya kawi.

Jeshi la Iran lilisema jana limetekeleza shambulizi la kombora na droni nchini Israel na kulenga ngome tatu za Amerika eneo hilo, likitaja mashambulizi hayo awamu ya kwanza ya kulipiza kisasi kwa wafanyakazi waliouawa katika maeneo ya viwanda Iran.

Jeshi la Israel lilisema linatibua mashambulizi yanayoilenga.

Saudi Arabia ilitibua na kuharibu droni 10 katika jiji kuu la Riyadh na Mashariki, wizara ya ulinzi ilisema.

Jeshi la Iran lilisema halikuhusika kwa vyovyote na shambulizi hilo, zilisema ripoti za kituo kisicho rasmi cha habari, Fars.

Katika muktadha huo, Trump pia ametishia kutekeleza mashambulizi zaidi kwenye Kisiwa cha Kharg, ambacho ni kituo kikuu cha mafuta nchini Iran, huku akiwahimiza wandani wake kuimarisha uwepo wa kijeshi katika eneo hilo wakati Tehran ikiapa kuzidisha ulipizaji kisasi.

Huku vita vya Amerika-Israel dhidi ya Iran vikiingia wiki ya tatu, Trump amesema mashambulizi ya angani yaliyotekelezwa na Amerika “yamesambaratisha kabisa” sehemu kubwa ya kisiwa hicho na kuonya kuhusu mashambulizi zaidi, akieleza shirika la habari la NBC Jumamosi, “Huenda tukailenga mara kadhaa zaidi kwa kujiburudisha tu.”

Mapigano hayo hayaonyeshi dalili zozote za kufika kikomo. Trump alisema Tehran yamkini iko tayari kuafikiana kuhusu mkataba wa kumaliza vita lakini kuwa “matakwa bado si bora ya kutosha.”