Ufichuzi: Wakenya wanapata kazi serikalini wakitumia vyeti feki
TUME ya Maadili na Kukabili Ufisadi (EACC) imepokea ripoti 853 kuhusu vyeti ghushi vya elimu tangu Januari 2023.
Miongoni mwake, visa 691 vinachunguzwa huku faili 182 zikikamilika na 27 kupatikana na hatia dhidi ya mbili zilizoondolewa mashtaka na moja iliyofutiliwa mbali.
Visa 60 vingali kortini, 41 vinasubiri kuangaziwa na Afisi ya Mashtaka ya Umma (DPP) na faili 51 zingali na Tume zikisubiri tathmini.
Takwimu hizo ni kionjo tu cha jinamizi linaloandama sekta ya ajira nchini ambalo limekataa kuondoka.
Kulingana na EACC, idadi hiyo huenda ikawa hata zaidi huku Tume ikisema Kenya kwa muda mrefu imekosa datakanzi ya raia wake walio na digrii, stashahada na vyeti na hivyo kufanya kuwa vigumu kwa waajiri kupiga msasa na kuthibitisha vyeti vya elimu vinavyomilikiwa au kuwasilishwa na wanaosaka ajira.
Katika ripoti yake mpya iliyoangazia kipindi kati ya Oktoba 1 na Disemba 31,2025 iliyotolewa Machi 6, 2025 – EACC ilithibitisha visa vinane, vitatu kutoka afisi ya Mkaguzi Mkuu (OAG).
Kisa kimoja kinahusu uchunguzi kuhusu madai ya kughushi dhidi ya naibu mkurugenzi wa ukaguzi katika OAG anayedaiwa kuwasilisha vyeti bandia vya elimu ili kupata nafasi ya msimamizi msaidizi wa ukaguzi.
Udadisi wa EACC ulibaini kuwa wakati wa kuteua makurutu kwa nafasi ya Msimamizi Msaidizi wa Ukaguzi, mshukiwa aliwasilisha cheti cha Shahada ya Taaluma kuhusu Biashara (Uhasibu), Kitengo cha Daraja la Pili kutoka Chuo Kikuu cha Mount Kenya alikosomea kutoka 2008 hadi 2010.
Hata hivyo, baada ya mchakato wa uthibitishaji, Msajili wa Elimu katika Chuo Kikuu cha Mount Kenya aligundua cheti hicho ni bandia na kwamba jina la mshukiwa halikuwa kwenye kijitabu cha mahafala.
Katika enzi yake ya ajira, mshukiwa alilipwa zaidi ya Sh28.4 milioni.
Fidia
Katika afisi iyo hiyo, msaidizi wa afisi aliwasilisha cheti ghushi cha KCSE kupata ajira na sasa EACC inataka kurejesha Sh3 milioni kutoka kwa mshukiwa.
Katika visa vingine, mshukiwa alibadilisha alama zake kutoka D hadi C ili kupata ajira kama afisa wa kliniki kwenye kitengo cha Huduma za Afya Chuo Kikuu cha Sayansi na Teknolojia cha Masinde Muliro.
Isitoshe, mshukiwa kamwe hakuhudhuria Chuo cha Mafunzo ya Matibabu (KMTC) licha ya kuwasilisha cheti cha Stashahahda katika Uuguzi wa Jamii.
“Hivyo basi, nambari ya usajili ya Uuguzi Kenya KRCHN1403 ni bandia vilevile. Kwa kipindi cha ajira katika Chuo Kikuu cha Masinde Muliro, mshukiwa alipokea Sh7,584,574 kama mshahara,” ilisema EACC katika ripoti.
Kisa kingine kilihusisha Katibu Msaidizi katika Bunge la Kaunti ya Trans Nzoia kughushi shahada ya digrii katika Usimamizi wa Biashara kutoka Chuo Kikuu cha Kisii.
Alitumia digrii hiyo ghushi kutuma maombi ya kuhamishwa kutoka wadhifa wa msimamizi wa afisi hadi kuwa afisa wa usimamizi lakini baadaye akafutwa kazi.
EACC ilimudu kushtaki wahusika 50 tu kati ya 2020 na 2026 huku sehemu kubwa (28) ikifichuliwa mnamo 2025.