Mbai afichua alivyoagizwa kumlinda Kivuitu akitangaza matokeo tata 2007
MBUNGE wa Kitui Magharibi Nimrod Mbai amefichua jinsi serikali ilivyompa silaha kuhakikisha anampa ulinzi mkali aliyekuwa Mwenyekiti wa Tume ya Uchaguzi (ECK) marehemu Samuel Kivuitu wakati wa uchaguzi tata wa 2007.
Bw Mbai wakati huo alikuwa mlinzi wa Waziri wa Leba, Dkt Alfred Mutua ambaye alikuwa wakati huo Msemaji wa Serikali ya Rais Mwai Kibaki.
Mbunge huyo alifichua kuwa aliitwa na Dkt Mutua katika jengo la KICC ambako kura zilikuwa zikihesabiwa na kupewa maagizo ya kumlinda Bw Kivuitu kwa sababu kulikuwa na hatari ya ghasia kuzuka.
Alifichua kuwa pamoja na Bw Mutua na maafisa wengine wa ngazi ya juu serikali, walikutana na Bw Kivuitu ambako walielewana kuwa angetamka tu jina la kijiji cha Ukambani basi mwenyekiti huyo angeondoka KICC kwa sababu za kiusalama.
Ukumbi wa KICC wakati huo ulikuwa umesheheni taharuki kati ya mirengo ya ODM na PNU kuhusu nani alikuwa mshindi wa kura za urais 2007.