Habari za Kitaifa

Ruto atua Magharibi kufifisha umaarufu wa kina Sifuna, Natembeya

Na RUSHDIE OUDIA March 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

RAIS William Ruto jana alianza ziara ya siku tano Magharibi mwa Kenya akilenga kuimarisha uungwaji mkono wake katika eneo hilo na kuzima umaarufu wa upinzani uchaguzi mkuu wa 2027 ukikaribia.

Katika ziara hiyo, Rais atazitembelea kaunti za Busia, Bungoma, Kakamega na Vihiga akisaka kurithi ufuasi ambao marehemu Raila Odinga alikuwa akijivunia.

Baadaye, kiongozi wa nchi atakuwa katika eneo la Gusii kuanzia Machi 29 hadi 31 akitembelea kaunti za Nyamira na Kisii.

Akiwa Kisii, Rais atatoa basi la kisasa kwa kikosi cha Shabana kinachoshiriki Ligi Kuu ya Kenya (KPL).

Pia atazindua barabara kadhaa na mradi wa kuunganisha umeme katika maeneo mbalimbali, na miradi ya ujenzi wa nyumba za gharama nafuu mbali na miradi mingine.

Ziara ya Rais inajiri majuma machache baada ya upinzani kukita kambi katika eneo la Gusii na kuwataka wakazi wapige kura za kumng’atua Dkt Ruto madarakani mwaka ujao.

Aliyekuwa Waziri wa Usalama wa Ndani Dkt Fred Matiang’i aliwaongoza vinara wenzake katika ziara ya siku nne Gusii mapema mwezi huu.

Magharibi, Rais Ruto anasaka uungwaji huku chama cha ODM ambacho kimetawala siasa za eneo hilo kwa miaka mingi, kikitikiswa na mgawanyiko.

Wiki chache zilizopita kundi la Linda Mwananchi ambalo linaongozwa na Katibu wa ODM Edwin Sifuna liliandaa misururu ya mikutano Busia, Vihiga na Kakamega na kuwarai wapigakura wasimchague Rais 2027.

Bw Sifuna, Mbunge wa Embakasi Mashariki Babu Owino, Gavana wa Siaya James Orengo na Naibu Kiongozi wa ODM Godfrey Osotsi walimshutumu Rais kwa kutokamilisha utekelezaji wa Agenda 10 kwenye muafaka wake na marehemu Raila Odinga mnamo Machi 7, 2025.

Rais alitua Kakamega mnamo Jumapili jioni na kukagua uwanja mdogo wa ndege wa Kakamega ambao umekuwa ukifanyiwa ukarabati alikofuatilia shughuli za upanuzi wake.

Jana, Rais alizindua ujenzi wa barabara ya Nangina-Sio Port-Okados-Mundere katika Kaunti ya Busia. Mradi huo wa Sh860 milioni utaunganisha maeneobunge ya Funyula na Budalang’i na pia kufungua eneo hilo kiuchumi.

Bado akiwa Busia aliweka jiwe la msingi kwa ujenzi wa soko la kisasa la Budalang’i ambalo litajengwa kwa Sh130 milioni kisha pia akazindua ujenzi wa barabara ya Matayos-Namusira-Nasewa katika eneobunge la Matayos.

Rais alifululiza hadi kijiji cha Nderema eneobunge la Mumias Mashariki, Kakamega ambako alizindua mradi wa kuunganisha umeme katika nyumba 161 kwa kima cha Sh12.7 milioni.

Alizindua ujenzi wa soko la Malaha kwa Sh270 milioni, mradi huo ukiwa ni kati ya masoko 24 yanayojengwa na serikali kuu katika kaunti mbalimbali nchini kwa gharama ya Sh4.4 bilioni.

Katika eneobunge la Ikolomani, Rais alizindua mradi wa maji wa Shitoli unaolenga kuwapa wakazi zaidi ya 45,000 maji safi.

Mradi huo unaendeshwa na Kampuni ya Maji ya Ziwa Viktoria.

Baada ya Kakamega, Rais alipaa angani hadi Kaunti ya Vihiga, ambapo alizindua ujenzi wa barabara ya Chavaki-Lusiolo na Shikumu-Malinya Sh953 milioni.

Rais kila mara akihutubu alionekana kutumia miradi anayozindua kuwakabili wapinzani wake.

“Tuna rekodi nzuri ya kutimiza ahadi kwenye sekta ya afya, elimu, barabara na nyumba za gharama nafuu. Kote nchini tunabadilisha maisha ya Wakenya kwa kuwa miradi ya maendeleo bila kumwacha mtu yeyote nyuma,” akasema Rais Ruto.

Alisisitiza kuwa hasumbuliwi na wapinzani wake ‘wanaopiga kelele’ akisema miradi ya mabilioni aliyoanzisha inalenga kubadilisha nchi kiuchumi.

“Wakenya si wajinga na wanaweza kuona kile tumefanya. Wakati ukija, wataamua nani ameendeleza nchi kwa kuangalia rekodi yake,” akaongeza.

Baadhi ya viongozi ambao waliandamana na Rais ni magavana Paul Otuoma (Busia), Wilber Ottichilo (Vihiga), Fernandez Barasa (Kakamega) na wabunge kutoka jamii ya Mulembe.

Mawaziri Wycliffe Oparanya (Waziri wa Vyama vya Ushirika na Biashara Ndogondogo), Alice Wahome (Ardhi na Nyumba) miongoni mwa viongozi wengine.

Kiongozi wa nchi pia aliwaomba wananchi waunge mkono ushirikiano wake na ODM akisema kuwa hawezi kukubali eneo la Magharibi kusalia nyuma kimaendeleo.

Mnamo Jumamosi, Rais ataungana na mwenzake wa Uganda Yoweri Museveni katika kuzindua ujenzi wa reli ya kisasa SGR kutoka Naivasha hadi Kisumu.