Akili Mali

Jinsi ‘YouTube’ ilimpa wazo la ufugaji nyuki na kumgeuza mfanyabiashara hodari

Na WYCLIFFE NYABERI March 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

KIJIJI cha Bobaracho, eneobunge la Nyaribari Chache, Kaunti ya Kisii kina mradi mzuri wa ufugaji nyuki.

Mradi huo unamilikiwa na Peter Mautia, 24, ambaye aliuanzisha baada ya kutazama video moja kwenye mtandao wa YouTube.

Jarida la Akilimali lilipata fursa ya kutangamana na Mautia kufahamu mengi katika ufugaji huu.

“Nilikuwa nikitazama video kwenye simu yangu wakati kipindi cha mkulima kutoka Kaunti ya Nyeri kilipojitokeza. Alikuwa kijana kama mimi, ambaye alikuwa akieleza jinsi ufugaji nyuki ulivyomuinua kutoka kwa ukosefu wa kazi hadi kufikia hatua ambayo hakuwa na ndoto ya kutafuta kuajiriwa popote. Nilichochewa na uzoefu wake kuanzisha biashara yangu ya ufugaji nyuki miaka miwili iliyopita,” Mautia anasema.

Kabla ya kuanza biashara yake ya ufugaji nyuki, Mautia anasema, alifanya utafiti wa kisawasawa kuhusu nyuki hasa katika utambuzi wa mizinga ifaayo.

“Nilifanya utafiti na kugundua kuwa kuna aina tofauti za mizinga ya nyuki ambayo hutumiwa katika kilimo hiki. Nilipima faida na hasara za kila aina ya mzinga kabla ya kuamua kutumia mizinga ya Langstroth,” Mautia anasema huku akiongeza kuwa aina hii ya mizinga huchukua muda mfupi kuvuna ikilinganishwa na mizinga mingine.

Mnamo Februari 2023, alinunua mizinga mitano na kuiweka kwenye uwanja wazi katika shamba la wazazi wake.

Alipata kila mzinga kwa gharama ya Sh5,000 kila mmoja.

Ndani ya majuma machache baada ya kuwekwa, mizinga yake yote ilitawalwa na nyuki. Baada ya miezi sita, Mautia alifanya mavuno yake ya kwanza.

“Nilipata kilo 40 za asali kutoka kwa mizinga yangu mitano. Niliuza kila kilo kwa Sh1,000 na kugundua kuwa nimepata faida ya Sh15,000 baada ya kuondoa gharama zote nilizotumia kuanzisha mradi huo,” anasema.

Baada ya kuhakikisha kuwa ufugaji wa nyuki ni biashara yenye manufaa, Mautia alitamani kufanya makubwa katika hilo.

Mwanzoni mwa mwaka 2025, aliongeza idadi ya mizinga yake ya nyuki. Pia alijenga nyumba ya nyuki ili aweze kuweka mizinga yake yote kwa usalama.

Kwa kutumia baadhi ya hela za akiba yake, alijenga nyumba ndogo ya nyuki iliyomgharimu Sh25,000.

Badala ya kununua mizinga mingine wakati huu, alichagua njia ya gharama nafuu kwa kununua mbao, na malighafi mengine yanayohitajika kutengeneza mizinga.

Kisha alimtafuta seremala akamtengenezea mizinga hiyo kwa bei nafuu. Kutokana na hili, Mautia alitengeneza mizinga 25 mipya ambayo alitumia kupanua ufugaji wake wa nyuki.

Ukiongeza ile mitano aliyoanza nayo, sasa anajivunia mizinga 30 ambayo ameiweka katika nyumba yake ndogo ya nyuki iliyotengenezwa kwa mbao na mabati.

Mizinga 23 tangu wakati huo imetawaliwa na nyuki huku saba ikiwa bado.

Tangu kupanua ufugaji wake, Mautia hukusanya zaidi ya kilo 100 kwa mwaka. Anauza asali yake kwa majirani na maduka lakini anasema soko ni pana kiasi kwamba hawezi kukidhi mahitaji yake.

Baadhi ya wakulima kijijini mwao wameanza kuvutiwa na ufugaji wa nyuki kama wa Mautia.

Kwa kuwa wakulima hawa bado hawana ujuzi wa nyuki, Mautia amekuwa akitumia fursa hiyo kujichumia riziki zaidi kutoka kwao.

Anahoji kuwa baadhi ya wakulima hao humtaka awauzie mizinga ambayo tayari ina nyuki.

Mwezi jana pekee, Bw Mautia alimuuzia mkulima mmoja mizinga mitatu yenye nyuki kwa Sh10,000 kila mmoja.

Ili kuhakikisha kuwa nyuki wake wanazalisha asali zaidi, Mautia amepanda alizeti karibu na eneo lake la kuwafugia nyuki ili wakusanye nekta kutoka ya kutosha, inayosaidia katika kuunda asali.

Hata hivyo anasema kama ilivyo kwa biashara nyingine ufugaji nyuki una changamoto zake na endapo mkulima atashindwa kuzipunguza basi atapata hasara kubwa.

“Kuna baadhi ya wadudu ambao wanapenda kushambulia nyuki kwenye mizinga. Wadudu hawa hula asali na wanaweza kuwafukuza nyuki kwenye mzinga iwapo kuna shambulio kubwa,” anasema, akiongeza kuwa ukaguzi wa mizinga mara kwa mara na usafi utasaidia kukabiliana na tatizo hilo.

Changamoto nyingine ni sumu kwa nyuki.

“Siku hizi, watu wengi wananyunyizia mimea yao dawa za kuua wadudu zaidi hasa inapochanua, kwa mfano maharagwe. Nyuki wanapofika kwenye maharagwe hayo ili kunyonya nekta, utagundua kuwa dawa iliyopulizwa kwenye mmea inawadhuru na kwa utaratibu huo, idadi ya nyuki wako itapungua kwa kiasi kikubwa.”