Gachagua atamlemea Ruto katika uchaguzi wa Ol Kalou?
ALIYEKUWA Naibu wa Rais Rigathi Gachagua amechukua udhibiti wa siasa za Ol Kalou baada ya mchujo wa chama chake cha DCP kuchangamkiwa na wapigakura wengi kuliko UDA.
Bw Gachagua alipuuza ombi la Jubilee la kutowasilisha mwaniaji kwa wadhifa huo uliokuwa ukishikiliwa na marehemu David Kiaraho kwa tikiti ya chama hicho.
Bw Gachagua amesema kuwa ushindani huo ni wa kirafiki kati ya vyama katika muungano wa upinzani.
Kutokana na idadi ya wapigakura waliojitokeza kwenye mchujo huo, Bw Gachagua amethibitisha kuwa DCP ina ufuasi mkubwa zaidi eneo hilo.
Hii ni kwa sababu idadi ya waliojitokeza kushiriki mchujo huo mnamo Jumamosi ni wengi kuliko wale waliojitokeza kwenye mchujo wa UDA mnamo Ijumaa.
Kati ya wapigakura 72,997 waliosajiliwa katika eneobunge hilo, wapigakura 23,763 walijitokeza kushiriki mchujo wa DCP, sawa na asilimia 32.6 ya waliojiandikisha.
Hii ni tofauti kubwa ikilinganishwa na kura watu 8,215 walioshiriki mchujo wa UDA, sawa na asilimia 11.3 pekee ya wapigakura waliosajiliwa.
Bw Samuel Kamau Ngotho wa DCP aliibuka mshindi kwa kupata kura 12,947, na sasa atakabiliana na Muchina Nyaga wa UDA, ambaye alishinda katika uteuzi wa chama chake kwa kura 3,221.
Bw Ngotho alifuatwa na Paul Waiganjo, aliyepata kura 4,978, huku Peter Mwangi akimaliza wa tatu kwa kura 3,919, idadi ambayo pia ni juu kuliko kura zote alizopata mshindi wa UDA katika mchujo.
Kwa namna ambavyo DCP iliendesha mchujo wake, inaonekana wazi kuwa Bw Gachagua alikuwa na malengo makubwa zaidi.
Alitaka kutumia nafasi hiyo kuonyesha nguvu zake kisiasa pamoja na kujaribu mfumo wake wa uchaguzi uliopangwa kwa ustadi mkubwa kwa ajili ya michujo ya 2027.
Kwa upande wa teknolojia, wakati UDA ikichukua zaidi ya saa saba kuhesabu, kuthibitisha na kutangaza matokeo ya kura 8,215 pekee, DCP ilichukua saa tano kufanya shughuli hiyo na kutangaza matokeo kufikia saa tano usiku.
Hii ni licha ya kuwa DCP ilitumia mfumo wa kupiga kura wa kawaida katika vituo vya kupigia kura.
Kwa upande mwingine, UDA ilikuwa imewekeza pakubwa katika vifaa vya kielektroniki vya kupigia kura ambapo matokeo yalikuwa yakipeperushwa moja kwa moja.
Hata hivyo, chama hicho kilitangaza matokeo yake baada ya saa sita usiku, karibu saa saba baada ya kufungwa rasmi kwa upigaji kura.
DCP pia ilikuwa imewekeza pakubwa katika vibanda vya kupigiakura vya chuma, jambo ambalo ni changamoto kubwa kwa Tume Huru ya Uchaguzi na Mipaka (IEBC), ambayo kwa kawaida hutumia vibanda vya makatoni.
Baada ya kura kuhesabiwa kwa mkono katika vituoa, matokeo yalihifadhiwa kwa njia ya kielektroniki na kuingizwa rasmi katika mfumo wa chama baada ya kuthibitishwa na wadau wote katika kituo cha kujumlisha kura.
DCP ilitoa matokeo kwa njia ya mfumo maalumu wa kidijitali kupitia programu maalum ya simu.
Ufanisi katika usimamizi wa muda ulikuwa sehemu muhimu ya mchakato huo, huku vifaa vyote vya uchaguzi vikifika katika vituo kufikia saa 11 alfajiri Jumamosi, na vifaa vyote kurejeshwa katika kituo cha kujumuisha kura kufikia saa 3 usiku baada ya shughuli ya upigaji kura kukamilika.
Kwa upande wa UDA, baadhi ya masanduku ya kura yalikuwa bado hayajafika katika kituo cha kuhesabia kura cha Mumbi kufikia saa 4 usiku, hasa kutoka wadi za Kanjuiri na Mirangine.
Ni kura kutoka wadi hizo mbili ambazo mgombea wa UDA, George Wambugu anazitumia kama ushahidi wa madai ya uchakachuaji wa uchaguzi katika kesi aliyowasilisha mbele ya mahakama ya chama hicho.
Naibu kiongozi wa DCP, Cleophas Malala ambaye amekuwa mkosoaji mkuu wa serikali pia aliwasifu maafisa wa polisi kutokana na jinsi walivyosimamia mchujo wa Jumamosi. “Tuna furaha sana na namna polisi walivyowajibika leo. Natumai wataendelea hivyo hivyo wakati wa uchaguzi mdogo wa Julai 16 na hata katika uchaguzi mkuu wa mwaka ujao,” akasema.