Habari

Mwanaharakati awasilisha kesi kupinga bei mpya ya mafuta

Na WINNIE ONYANDO May 17th, 2026 Kusoma ni dakika: 1

MWANAHARAKATI Francis Awino amewasilisha kesi katika Mahakama Kuu jijini Nairobi kupinga ongezeko jipya la bei ya mafuta lililotangazwa na Mamlaka ya Kudhibiti Kawi na Petroli nchini (EPRA) mnamo Mei 14, 2026.

Katika kesi hiyo iliyowasilishwa chini ya Kitengo cha Katiba na Haki za Kibinadamu, Awino anadai kuwa ongezeko hilo ni mzigo mkubwa kwa Wakenya na limekiuka haki za wananchi kikatiba kutokana na ukosefu wa uwazi na ushirikishwaji wa umma.

Kulingana na stakabadhi za mahakama, EPRA mnamo Mei 14, 2026 ilitangaza kuwa bei ya petroli iliongezeka kwa Sh16.65 kwa lita huku dizeli ikipanda kwa Sh46.29 kwa lita.

Awino anasema ongezeko hilo limeathiri pakubwa wananchi, hasa magari ya uchukuzi, wakulima, wafanyabiashara wadogo na familia zinazotegemea bidhaa zinazohusiana na mafuta.

Rais wa Bunge la Mwananchi Francis Awino akihutubia wanahabari Nairobi. PICHA|WINNIE ONYANDO

Aidha, anahoji matumizi ya zaidi ya Sh5 bilioni kutoka Hazina ya Petroleum Development Levy Fund yaliyolenga kupunguza mzigo wa bei ya dizeli na mafuta ya taa, akitaka serikali kueleza namna fedha hizo zilitumika.

Katika kesi hiyo, mwanaharakati huyo pia amelalamikia hatua ya serikali kuruhusu kwa muda matumizi ya mafuta yenye kiwango cha juu cha salfa, akisema hatua hiyo inaweza kuhatarisha afya ya wananchi na mazingira.

Awino anasema serikali ilitangaza kupunguza ushuru wa VAT kwa bidhaa za petroli hadi asilimia nane mwezi Aprili mwaka huu, lakini wananchi hawajafaidika kutokana na hatua hiyo.

Kupitia ombi la dharura lililowasilishwa mbele ya Mahakama Kuu ya Milimani, Awino anaitaka mahakama iingilie kati haraka ili kusitisha utekelezaji wa maamuzi hayo huku akionya kuwa gharama ya juu ya mafuta inaweza kusababisha maandamano na hali ya taharuki nchini.

Haya yanajiri huku maandamano yakitarajiwa kufanyika kesho kupinga ongezeko la bei ya mafuta nchini