Tahariri

TAHARIRI: Rais atumie ziara kuanika mafanikio yake

Na MHARIRI MKUU March 18th, 2026 Kusoma ni dakika: 2

RAIS William Ruto wiki hii yumo ziarani katika eneo la Magharibi mwa nchi ambapo amekuwa akizindua miradi ya maendeleo huku pia akisaka uungwaji mkono kuelekea uchaguzi wa 2027.

Hii si mara ya kwanza Rais Ruto anazuru kaunti za Kakamega, Busia, Bungoma na Vihiga tangu achaguliwe mnamo 2022.

Mara kwa mara, Rais anapozuru eneo huwa anafuatilia miradi iliyoanzishwa, ile iliyokamilishwa na ile inayozinduliwa.

Kwa hivyo, katika ziara hii, Rais anastahili kuwaeleza wakazi kile ambacho serikali yake imefanya hata anapofungua miradi mipya.

Mnamo Machi 21, 2024 wakati wa Kongamano la Uwekezaji Kaunti ya Kakamega, Rais Ruto aliahidi kufufua sekta ya sukari kwa kukodisha viwanda vya sukari Magharibi na Nyanza.

Kwa miaka mingi uti wa mgongo wa uchumi wa Magharibi ulikuwa ni kilimo cha miwa na Kiwanda cha Sukari cha Mumias.

Mwishowe viwanda hivyo vilikodishwa kwa wastawishaji wa kibinafsi lakini mabadiliko ya maana bado hayajaonekana.

Kiwanda cha Mumias na viwanda vingine bado vinakabiliwa na changamoto tele huku wakulima wakilalamikia kucheleweshewa malipo.

Aidha, kuna madai baadhi ya wamiliki wapya wa viwanda hivi wanawanyanyasa wafanyakazi wao na hata bonasi hawalipi.

Rais Ruto alikuwa ameahidi kwamba viwanda vya Nzoia, Sony, South Nyanza na Chemelil vingepokea jumla ya Sh5.23 bilioni mnamo Julai mwaka jana.

Kile ambacho wengi wanataka kufahamu ni iwapo pesa hizo zilizolenga kumaliza madeni ya wafanyakazio zilitolewa na matumizi yao kuwekwa paruwanja.

Swali ni je, kuna mabadiliko katika sekta ya kilimo cha miwa au uzalishaji wa sukari tangu Rais Ruto aingie mamlakani na ahadi zote amezitimiza?

Kuhusu nyumba za gharama nafuu angalau serikali imekuwa ikionyesha ufanisi wake na kusema idadi ambayo imekamilika, zile zinazojengwa na zile ambazo zinazinduliwa.

Ni raha sana kuona Rais akifungua zile ambazo zimekamilika huku akiahidi Wakenya makazi bora wakati wa utawala wake.

Pia Rais aeleze kulikofikia ujenzi na ukarabati wa nyuga mbalimbali ikiwemo Bukhungu na Kanduyi.

Bukhungu imekuwa ikikarabatiwa kwa kipindi kirefu na ni kati ya nyuga ambazo zitatumika kwa mazoezi na timu zitakazoshiriki Kombe la Afrika mwaka ujao.

Je, ukarabati wa uga wa Kanduyi umefikia wapi tangu iandae Sherehe za Madaraka mnamo Juni 1 2024.

Je, mwanakandarasi alitaliki shughuli za ukarabati jinsi ambavyo imekuwa ikidaiwa?

Ziara hii ya Ruto iwe tofauti na ijikite sana katika miradi iliyokamilishwa badala tu ya siasa za ubabe.