Siasa

Winnie Odinga ang’ang’ania na makundi pinzani ya Oburu na Sifuna

Na MOSES NYAMORI March 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

MBUNGE wa Jumuiya ya Afrika Mashariki (EALA) Winnie Odinga anaonekana kung’ang’aniwa na mirengo miwili ndani ya ODM kufuatia pendekezo awe naibu kiongozi wa chama cha Orange Democratic Movement (ODM) chini ya mjomba wake Dkt Oburu Oginga.

Ndani ya mrengo wa Linda Ground wa chama hicho unaoongozwa na Dkt Oburu, pendekezo hilo limezua mgawanyiko wakosoaji wakisema ni wazo “baya” na linaweza kukifanya chama hicho kionekane kama mali ya familia moja.

Wanachama wa mrengo wa Linda Mwananchi unaoongozwa na Katibu Mkuu Edwin Sifuna wasema pendekezo hilo limechukuliwa kama hatua ya kuudhoofisha.

Hata hivyo, wanaounga mkono pendekezo hilo wanasema kumteua Winnie kama mmoja wa manaibu wa kiongozi wa chama kutaleta nguvu mpya na kuwapa vijana nafasi katika uongozi wa juu wa chama hicho.

Wanaounga mkono pia wanasema Winnie anafaa kuhukumiwa kwa uwezo wake wa uongozi, wala si kwa sababu ya ukoo wake wa kisiasa.

Lakini wakosoaji wanasisitiza kuwa na watu watatu kutoka familia ya Odinga katika ngazi ya juu ya uongozi wa ODM kutaharibu taswira ya chama hicho kitaifa, iliyojengwa kwa zaidi ya miaka 20.

Wanasema hali hiyo pia itatoa ujumbe mbaya kwamba uongozi wa chama ni urithi wa kifamilia.

Kwa mujibu wao, ili ODM ifanikiwe baada ya enzi za Raila Odinga, ni lazima chama hicho kijitanue zaidi ya familia ya Odinga.

Wanasema Winnie na hata Dkt Oginga hawana haki ya moja kwa moja ya kuongoza chama hicho.

Wakosoaji hao pia wanaeleza kuwa ODM ni chama cha kitaifa na hivyo, viongozi wake wakuu wanapaswa kuchaguliwa kutoka maeneo mbalimbali ya nchi ili kuonyesha sura ya Kenya nzima.

Iwapo pendekezo hilo litaidhinishwa katika mkutano wa kitaifa wa wajumbe wa chama utakaofanyika Machi 27, basi Dkt Oginga atakuwa kiongozi wa chama huku Winnie akichukua nafasi ya naibu kiongozi wa chama.

Wakati huo huo, Mwakilishi wa Wanawake wa Kisumu Ruth Odinga atakuwa naibu katibu wa mipango ya chama.

Viongozi hao watatu watakuwa wanachama wa Kamati Kuu ya Kitaifa ya chama (NEC), ambayo ndiyo chombo kikuu cha kufanya maamuzi katika ODM.

Aidha, Dkt Oginga na Winnie pia watakuwa wanachama wa Kamati ya Usimamizi ya chama.

Iwapo Winnie ataingia katika safu ya juu ya uongozi, Kaunti ya Siaya itakuwa na angalau viongozi wanne wa kitaifa ndani ya ODM.

Mbunge wa Rarieda Otiende Amollo pia ni mwanachama wa NEC kama naibu mwenyekiti wa chama.

Pendekezo hilo pia litapanua nyadhifa za kitaifa kwa kuongeza manaibu wanne wa kiongozi wa chama.

Kwa sasa, Gavana wa Mombasa Abdulswamad Nassir, Gavana wa Kisii Simba Arati na Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi wanahudumu kama manaibu wa kiongozi wa chama.

Baadhi ya wanachama wa ODM waliozungumza na wanahabari walipinga wazo hilo lakini wakaomba majina yao yasitajwe kwa kuhofia kuonekana kama wanapinga familia ya Odinga.

Kwa upande mwingine, baadhi ya wanachama wa mrengo wa Linda Mwananchi wanasema pendekezo hilo linaweza kuwa sehemu ya njama ya kudhoofisha mrengo pinzani ndani ya chama.

Kwa muda mrefu, Winnie amekuwa akihusishwa na mrengo wa Katibu Mkuu wa ODM Edwin Sifuna.

Kuonekana kwake katika mkutano ulioitishwa na mwenyekiti wa ODM Nairobi na Mbunge wa Makadara George Aladwa kulifasiriwa kama ishara ya mabadiliko ya msimamo wake kisiasa.

Hata hivyo, Bw Aladwa alitetea pendekezo hilo akisema ni hatua muhimu ya kuimarisha umoja ndani ya ODM kuelekea uchaguzi mkuu wa 2027.

“Winnie ni mtu huru na ana haki ya kuwania wadhifa wowote wa uongozi ndani ya chama. Hatuwezi kumzuia kugombea kwa sababu ya uhusiano wake na Oburu. Tunahitaji vijana zaidi katika uongozi wa chama,” alisema Bw Aladwa.

Mbunge wa Gem Elisha Odhiambo pia aliunga mkono wazo hilo akisema litasaidia kuipa ODM nguvu mpya kwa kuwashirikisha vijana katika uongozi wa chama.

Katika hotuba yake wakati wa mkutano uliofanyika katika Jaramogi Oginga Odinga Foundation (JOOF), Winnie alisema ataendelea kubaki ndani ya ODM.

“Hiki ni chama chetu, nyumba yetu. Ni nyumba ambayo baba yangu alijenga. Naweza kuondokaje hapa? Nitabaki ODM,” alisema.

Hata hivyo, Mbunge wa Kileleshwa Robert Alai alikosoa kauli hiyo akisema inachochea dhana kwamba ODM ni urithi wa familia.