Jinsi mhandisi alivyogeuka mkulima na kujenga himaya ya kanga na kuku
KILOMITA chache kutoka mji wa Kitengela, Kaunti ya Kajiado, mfugaji mmoja anaonekana kubadilisha taswira ya dhana ya eneo hilo linalojulikana kama kame (ASAL).
Kajiado, ni maarufu kwa ufugaji wa ng’ombe wa nyama ikizingatiwa kuwa kiwango chake kikubwa cha ardhi kinamilikiwa na jamii ya Maasai ambayo ni ya kuhamahama.
Kwenye shamba la Fredrick Omondi, ubunifu katika sekta ya ufugaji kuku na ndege wa nyumbani umeshika kasi.
Omondi ndiye mwanzilishi wa Kimalat Holdings Ltd, na kilichoanza kama mapenzi tu ya ufugaji sasa kimegeuka kuwa himaya ya biashara ya kanga, kuku aina ya Brahma na ndege wa mapambo nyumbani.
Unapoingia kwenye mradi wake wa ekari moja, kitu cha kwanza kinachokuvutia si milio ya kawaida ya kuku, bali ni sauti za kutuliza moyo za mamia ya kanga wanaotembea huru.
Mwonekano wao wa kuvutia unaakisi ubunifu uliomfikisha hapo.
Akiwa mhandisi aliyebadili mwelekeo, Omondi alianza kutoka chini. “Nilianza na kanga 23 na kuku watatu wa Brahma, kwa mtaji wa Sh50,000 miaka mitatu iliyopita,” anafichua.
Leo hii, mradi wake una zaidi ya kanga 800, kuku 300 wa Brahma na takriban kuku 400 wa Kenbro, pamoja na ndege wa mapambo kama vile Japanese Silkie na Polish Bantam.

Anasema alichagua ufugaji wa kuku kwa sababu unahitaji nafasi kidogo tu na una faida kubwa, huku kanga wakimletea mabadiliko makubwa.
Alianza na kuku wa Kenbro lakini alikumbana na mikurupuko ya maradhi ambayo nusra izime ndoto zake. Hali hiyo ilimlazimu kutafuta njia mbadala, ndipo alipogundua kanga kupitia utafiti na mashauriano na wataalamu wa mifugo.
“Kanga ni bora—wana nguvu, hawaugui rahisi, hukua haraka na hawahitaji chakula kingi,” anakiri.
Biashara yake inaegemea sana uanguaji wa vifaranga wa kanga na kuwauza. Ana mbalimbali ya kanga kama vile wa rangi nyeupe, lavender, helmeted na royal purple.
Jozi moja – ya kanga wawili huuza kwa wastani wa Sh4,000, huku kanga mmoja akitaga hadi mayai 300 kwa mwaka. Ujuzi wake wa uhandisi, anasema umemsaidia kupanga na kusimamia mifumo ya mradi wake.
Amewekeza kwenye mifumo ya kisasa kunywesha ndege wake maji, mabanda yanayoruhusu hewa kuingia na mfumo unaowaruhusu ndege kujitafutia chakula katika kichaka kilicho karibu na mradi wake.

“Kuwaachilia huru kujitafutia malisho kunanisaidia kupunguza gharama ya chakula kwa kiwango kukubwa,” Omondi anaambia Akilimali Dijitali.
Isitoshe, mfumo huo unafanikisha kanga kujitafutia wadudu kama vile panzi, mchwa na vyakula vya asili. “Mbinu hii huru imepunguza gharama za uzalishaji kwa asilimia 70,” anasema.
Kimauzo, huuza karibu kanga 300 kwa mwezi, ndege hao wakimuingizia karibu Sh600,000. Pia, huuza kuku wa Brahma na Kenbro, huku ndege wa mapambo wakishabikiwa na wanaopenda kurembesha kwao na ndege wa umaridadi.
Jitihada zake zilitambuliwa mwaka uliopita kupitia Maonyesho ya Kilimo na Kibiashara Nairobi (ASK) 2025, ambapo jogoo wake wa Brahma, “The White Giant,” alishinda tuzo ya bingwa mkuu daraja la kuku.
Licha ya changamoto za awali kama magonjwa na ukosefu wa soko, Omondi sasa analenga kupanua mradi wake na kuanzisha kituo cha mafunzo kwa vijana.