Jamvi La Siasa

Itakuwa kibarua ODM kuwika ngome ya Mulembe baada ya kumtimua Sifuna

Na CECIL ODONGO July 19th, 2026 Kusoma ni dakika: 3

ODM sasa ina kibarua kudumisha umaarufu wake Magharibi mwa nchi baada ya kukamilisha mchakato wa kumwondoa Seneta wa Nairobi Edwin Sifuna kutoka wadhifa wake kama katibu mkuu.

Bw Sifuna ambaye anaegemea mrengo wa Linda Mwananchi pia alitimuliwa kama Kiranja wa walio wachache katika Bunge la Seneti wiki.

Kando na Bw Sifuna, Seneta wa Vihiga Godfrey Osotsi pia mnamo Mei alifurushwa kama naibu kiongozi wa ODM. Wawili hao walikuwa viongozi wakuu ODM Magharibi hasa baada ya aliyekuwa Gavana wa Kakamega Wycliffe Oparanya kujiunga na Baraza la Mawaziri mnamo Julai 2024.

Wakati wa uhai wa Kinara wa Raila Odinga, Magharibi ilikuwa ngome yake ya kisiasa huku ODM ikitwaa viti vingi eneo hilo.

Chama hicho kilitamba katika siasa za Busia, Vihiga na Kakamega ambako ilitwaa viti vingi huku ikilemewa tu Bungoma na Ford Kenya.

Kwenye kura za urais, Bw Odinga alikuwa akitamba na mnamo 2022 alimbwaga Rais Ruto katika kaunti za Trans Nzoia, Vihiga, Kakamega, Busia akilemewa tu katika Kaunti ya Bungoma.

Katika uchaguzi mkuu uliopita ODM ilitwaa viti 10 vya ubunge kati ya 12 Kakamega pamoja na ugavana na mwakilishi wa kike.

Kaunti jirani ya Vihiga ODM ilitwaa ugavana na useneta huku kule Busia ikiwahi viti vinne kati ya saba vya ubunge. Pia ODM ilitwaa ugavana na mwakilishi wa kike.

ODM ilipata kiti cha ubunge wa Saboti katika Kaunti ya Trans Nzoia. Kushinda viti vingi na kura za urais kulisababisha Raila na ODM itambe kisiasa magharibi mwa nchi.

Hata hivyo, baada ya kuondolewa kwa Bw Sifuna na Bw Osotsi katika nyadhifa zao, ODM inaonekana kukosa mnato Magharibi jinsi ilivyokuwa hapo awali.

Mnamo Alhamisi Bw Sifuna alidai kuwa ODM imekufa huku pamoja na Gavana wa Siaya James Orengo wakizindua misururu ya mikutano ya kisiasa kote nchini kupitia vuguvugu lao la Linda Mwananchi.

“Kwa masikitiko makuu ODM kwa sasa wapo mahali ambapo maamuzi yanayoathiri chama na wanachama wake hayatoki tena Orange House.

Maamuzi hayo na yale yaliyosababisha niondolewe kama kiranja wa wa wengi kwenye Bunge la Seneti yalifanyika katika ikulu ya Nairobi,” akasema.

Pia alifichua kuwa viongozi ambao kwa miaka mingi wamemuunga mkono Kinara wa ODM Raila Odinga wameamua kufanya kazi chini ya vuguvugu la Linda Mwananchi.

“Tulifanya kazi kwa miaka mingi kuhakikisha kuwa tunatimiza ndoto ambayo Raila alifanyia kazi. Umaarufu wa chama mashinani umefifia kwa sababu ya tamaa ya baadhi ya viongozi baada ya kifo cha Raila,” akaongeza.

Kauli ya Bw Sifuna inaashiria kuwa chama cha ODM imekufa huku akitarajiwa kujiunga na chama kipya cha kisiasa.

Kuhusu Magharibi, Bw Sifuna anatarajiwa kutawazwa kama msemaji eneo hilo mnamo Julai 26 katika mkutano utakaofanyika uwanja wa Posta Kaunti ya Bungoma.

Mkutano huo umechemsha siasa za Bungoma ikizingatiwa kulikuwa na minong’ono kuwa Mbunge wa Kimilili Didmus Barasa pia alikuwa amepanga mkutano eneo la Musikoma, kilomita chache kutoka eneo hilo.

Bw Sifuna na Bw Barasa huwa hawaonani uso kwa macho na wamekuwa na uhasama katika mikutano ya hadhara na hafla za mazishi. Bw Barasa ametangaza kuwa sasa mkutano wake hautafanyika.

Kabla ya kutawazwa kama msemaji wa jamii ya Mulembe Julai 26, Bw Sifuna atakuwa kaunti jirani ya Trans Nzoia pamoja na viongozi wa Linda Mwananchi ambao wanaunga azma yake ya kuwahi uongozi wa nchi.

Siasa za Bw Sifuna zimeonekana kufunika ODM Magharibi bila Raila baadhi ya viongozi wa chama hicho wakizomewa kwenye mikutano na matanga kila mara wanapomkosoa seneta huyo wa Nairobi.

Mwenyekiti wa ODM Kaunti ya Kakamega ambaye pia ni Gavana wa gatuzi hilo Fernandes Baraza anasisitiza kuwa chama ni imara na umaarufu wake bado upo.

“Tumekuwa tukifanya mikutano na tunapokolewa vizuri na wanaosema ODM imepoteza umaarufu watashanga chama kikitwaa viti vingi eneo hili.

Mtu mmoja akiasi chama hakumaanisha kuwa wengine pia wameenda,” akasema Bw Barasa ambaye anaegemea mrengo unaoongozwa na Seneta wa Siaya Dkt Oburu Oginga.

Kwa mujibu wa Mchanganuzi wa Masuala ya Kisiasa Lumala Masibo, umaarufu wa Bw Sifuna na kutokwepo kwa Raila kunaiacha ODM na kibarua kigumu cha kudumisha umaarufu wake Magharibi.

“Masaibu ya Sifuna na Osotsi yamesawiri viongozi wa sasa wa ODM kama wasiojali uungwaji mkono ambao walikuwa wakiupata Magharibi mwa nchi miaka ya nyuma. Pia wengi wanahisi huu ni wakati wa Nyanza kurejesha mkono kwa kumuunga mkono Bw Sifuna,” akasema msomi huyo.

Utafiti wa Infotrak uliofanywa wiki hii hata hivyo, ulionyesha ODM kama chama ambacho bado ni maarufu Magharibi kwa asilimia 32.