Vijana Afrika wataka mifumo jumuishi ya chakula kufungua ajira na ubunifu
VIJANA barani Afrika wanaendelea kushinikiza ajenda ya mifumo jumuishi ya chakula ili kufungua nafasi za ajira na ubunifu kwenye mtandao wa uchakataji mazao ya kilimo, wakitaka sekta hiyo kutambuliwa upya kama chanzo cha biashara na mabadiliko ya uchumi.
Wito huo ulitolewa mnamo Machi 14, 2026 jijini Kigali, Rwanda, wakati wa kongamano la kaulimbiu “Who Gets to Shape Africa’s Food Future?” likileta pamoja vijana wajasiriamali kwenye kilimo, watunga sera na washirika wa maendeleo kutoka kote barani.
Kongamano hilo lililoandaliwa na AGRA kwa ushirikiano na Global Citizen liliangazia umuhimu wa mifumo dhabiti ya chakula, hasa kusaidia kuboresha biashara kupitia bunifu za kisasa.
Ingawa kilimo kinaajiri idadi kubwa ya Waafrika, vijana wengi bado hukiona kama chaguo la mwisho badala ya njia ya kiuchumi yenye faida. Changamoto kama vile ukosefu wa mtaji, ardhi, masoko na huduma za usaidizi wa biashara zinaendelea kuwazuia wengi kuingia au kukuza biashara zao.

Waziri wa Kilimo na Raslimali za Mifugo wa Rwanda, Dkt Telesphore Ndabamenye, alihimiza vijana kuangalia kilimo kama njia ya kuunda utajiri, kuhakikisha usalama wa chakula na kuunda ajira.
“Huwezi kuuza kile usichonacho. Katika safari ya mifumo ya chakula, lazima kwanza tuhakikishe upatikanaji wa chakula. Chakula huleta fedha, na fedha huleta ajira,” alisema.
Aliongeza kuwa licha ya juhudi za washirika wa maendeleo kusaidia vijana, jukumu la kubadilisha sekta ya kilimo liko mikononi mwa vijana wenyewe. Akizungumza katika hafla hiyo, Ifeoma Chuks-Adizue wa Global Citizen alisema kongamano hilo liliunda jukwaa muhimu la vijana kupaaza sauti zao.
“Ni muhimu kuelewa changamoto ambazo vijana wanakumbana nazo ili kusaidia kufanikisha malengo yao,” Ifeoma akasema, akiahidi ushirikiano wa Global Citizen na AGRA kuboresha mifumo ya chakula na kujumuisha vijana.
Kwa upande wake, Nana Yaa Boakyewaa Amoah wa AGRA alisisitiza kuwa vijana ni nguzo ya mageuzi kwenye mifumo ya chakula barani Afrika.

Kupitia mpango wa YEFFA, AGRA inasaidia biashara za kilimo zinazoendeshwa na vijana kwa kuwapa mafunzo, huduma za biashara, ufadhili na kuwatafutia masoko pamoja na kushirikisha watunga sera kuboresha mazingira ya biashara.
Nchini Rwanda, juhudi hizi tayari zimezaa matunda, huku biashara zinazoongozwa na vijana zikizalisha nafasi 12,248 za ajira na kujumuisha vijana 649 wenye ulemavu.
AGRA, pia, ina uwepo wake Kenya ambapo inaendelea kupiga jeki wakulima maeneo tofauti nchini.
Mjadala kushirikisha vijana kwenye kilimo unajiri wakati ambapo athari za mabadiliko ya tabianchi zinazidi kuathiri mifumo ya chakula barani Afrika, zikihitaji suluhisho na ubunifu kuziangazia.